All posts by admin5

26-0315 Mahali Alipopachagua Mungu Pa Kuabudia

UJUMBE: 65-0220 Mahali Alipopachagua Mungu Pa Kuabudia

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bi. Yesu Kristo,

Hii ndiyo siku yenyewe. Huu ndio wakati wenyewe. Mungu alimtuma tai Wake mwenye nguvu duniani kumwita Bi. Yesu Kristo Wake atoke, kunena na kumwambia, “Wewe NDIYE niliyemchagua. Wewe NDIYE ninayempenda. Wewe ndiye Bibi-arusi Neno bikira Wangu Mkamilifu. Sisi ni MMOJA.”

Kuyasikia maneno hayo tu, mioyo yetu inaruka kwa furaha. Kuwazia, katika ulimwengu wote, pamoja na mamilioni na mamilioni yake ya watu, kuna Bi. Yesu Kristo MMOJA tu, na WEWE ndiye Huyo, YULE anayemjia.

Kuna mahali PAMOJA tu palipochaguliwa pa kuabudia. Kuna Ujumbe MMOJA tu mkamilifu uliochaguliwa. Kuna BIBI-ARUSI MMOJA tu MKAMILIFU aliyechaguliwa…NASI NDIO!!

Baba ana mahali PAMOJA peke yake alipopachagua pa kuabudia, Bwana Yesu Kristo; Yeye ni Neno. Leo, kuna mahali PAMOJA peke yake ambapo mauti ya kiroho haiwezi kupiga: Neno. Mauti haiwezi kulipiga Neno, kwa sababu ni Neno la Mungu lililo Hai.

Ufunuo kamili wa Neno hilo lililo Hai umefunuliwa kwa Bi. Yesu Kristo peke yake. Kuna mahali PAMOJA tu palipochaguliwa ambapo Bi. Yesu Kristo anaweza kwenda na kulisikia NENO KAMILIFU LIKINENWA. Kuna nabii MMOJA tu aliyechaguliwa kuwa Sauti ya Mungu. Kuna mahali PAMOJA tu ambapo Bi. Yesu anapoweza kwenda na kuisikia, BWANA ASEMA HIVI: KUBONYEZA PLAY.

Kutakuweko Nuru mnamo wakati wa jioni, mahali pekee alipopachagua Mungu pa kuabudia. Loo, Ujumbe huu umefika wapi, Yeye atafanya nini? Na katika siku yake itakuweko Nuru wakati wa jioni, na (nini?) kuwakaribisha watoto Wake wanaporudi nyumbani kwenye Nchi ya kweli ya ahadi, kwa ishara ile ile ya Nguzo ya Moto ambayo iliwaongoza wana wa Israeli kupitia nyikani.

Jinsi gani Bibi-arusi Wake anavyopaswa kuwa mwangalifu kuifuata na kuisikia Sauti ya Mumewe ikizungumza Naye. Kuna mahali PAMOJA tu tunapoweza kwenda na kuwa na hakika 100%. Kuna Sauti MOJA tu tuliyoiwekea kikomo chetu cha Milele.

Bi. Yesu Kristo anaamini kwamba Maneno anayoyasikia kwenye kanda ni Maneno ya Mumewe. Yeye anaamini Neno Lake halihitaji fasiri yoyote. Kwa hivyo, Yeye anaamini kuna mahali PAMOJA tu palipoandaliwa ambapo Yeye anapoweza kwenda na kusema AMINA kwa kila Neno, Sauti ya Mumewe iliyo kwenye kanda.

Kwa mara nyingine tena, Bi. Yesu Kristo, kutoka kote ulimwenguni, anaweza kusema, “Leo, Neno hili lililonenwa, linatimizwa”.

Mungu Mpenzi, huko chini kuvuka majangwa kule Tucson, huko mbali California, juu huko Nevada na Idaho, kwenda hadi Mashariki na kila mahali, chini huko Texas; wakati mwaliko huu unatolewa, watu wamekiketi katika—katika makanisa madogo, vituo vya mafuta, majumbani, wakisikiliza.

Umealikwa kuja kusikiliza pamoja na Maskani ya Branham saa 6:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(Ni saa 1:00 JIONI ya Afrika Mashariki) tunapomsikia Mungu akizungumza na Bibi-arusi Wake mteule, Ujumbe: “Mahali Alipopachagua Mungu Pa Kuabudia” 65-0220.

Ndugu Joseph Branham

Maandiko: Kumbukumbu la Torati 16:1 hadi 3.

26-0308 Leo Maandiko Haya Yametimia

UJUMBE: 65-0219 Leo Maandiko Haya Yametimia

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Uzao Mkuu Wa Kifalme,

Ule wakati ambao tumekuwa tukiusubiri kwa hamu na kuutamani umewadia. Tumewasili. Tunauona ukijifunua mbele ya macho yetu. Kila siku unabii unatimia, nasi tunaweza kusema: LEO MAANDIKO HAYA YAMETIMIA MBELE YA MACHO YETU.

Ni changamko la Ufunuo lililoje linalotukia kwa Bibi-arusi. Kwa kila Ujumbe tunaousikia, tunahisi ndani ya mioyo na roho zetu, ” Linawezaje kuwa kubwa zaidi ya hapa na la ajabu zaidi kuliko hivi, Bwana?” Ndipo Yeye anakuja miongoni mwetu kwa mara nyingine tena na kututia mafuta tunapoisikia Sauti Yake ikituita na kusema, “Wewe ni Kipenzi Changu. Nilikuchagua wewe uwe Bibi-arusi Wangu. Kama vile nilivyokuahidi, ninakuja kukuchukua. Niko njiani. Hivi karibuni Tutakuwa pamoja milele.”

Tunapaza sauti kutoka kote ulimwenguni, tukivumisha Mbingu kwa haleluya zetu, utukufu, sifa, na kuabudu kwetu Kwake. Shetani ameshindwa. Baba ameyaondolea mbali mashaka yetu yote, kutokuwa na uhakika kwetu kote, kudhania kote. Tunaweza kutangaza kwa mioyo na roho zetu zote, SISI NDIO ule Uzao Mkuu wa Kifalme wa Ibrahimu. Bibi-arusi wa Kifalme kwa Mwana yule wa Kifalme aliyeahidiwa.

Uwepo wa Bwana umekuwa wa ajabu mno kwa anavyotufunulia Neno Lake kuliko hapo awali. Yeye amemuunganisha Bibi-arusi Wake pamoja na Neno Lake, na kutuweka katika Nia moja kwa umoja kama jamii moja, tukiisikiliza Sauti ya Mungu ikinena na kutukamilisha kwa Neno Lake.

Kila Ujumbe tunaousikia ni kama vile kisima kinachofoka maji kinachofurika ndani ya nafsi zetu; kikitiririka, kikisukuma, na kububujika kutoka kwenye Kiti cha Enzi cha Mungu. Tunakunywa, kunywa na kunywa, yakiziburudisha nafsi zetu.

Ndugu na Dada zangu, sisi ndio utimilifu wa Maandiko yanayosema Yeye atakuwa na Bibi-arusi Neno bikira. Sisi ndio: Leo Maandiko haya yametimia.

Mungu Mwenyewe alinena kutoka Mbinguni na malaika Wake wa saba na kusema, “Kama vile Yohana Mbatizaji alivyotumwa kutangulia Kuja kwa kwanza kwa Kristo, Ujumbe wako utatangulia Kuja Kwake kwa pili, duniani kote.” Bibi-arusi anaweza kusema: Leo Maandiko haya yametimia.

Je, hivi tunaweza kuelewa kwamba Sauti ya Mungu halisi imenena katika siku yetu kupitia midomo ya mwanadamu, ikarekodiwa, ikahifadhiwa, na kutunzwa ili Yeye aweze kunena na kila mmoja wetu, Bwana Asema Hivi? Yeye ameliwezesha hilo ili tusichukue neno la mtu yeyote, mawazo ya mtu yeyote, fikra za mtu yeyote, ni sisi kuketi tu na kuisikiliza Sauti Yake ikinena nasi moja kwa moja Neno Lake Safi.

NI KITU GANI KINACHOTENDEKA LEO?

Na M-w-a-n-a yule yule wa Mungu aliyetokea mashariki na kujithibitisha Mwenyewe kama Mungu aliyefanyika mwili, ndiye M-w-a-n-a yule yule wa Mungu aliyeko katika kizio cha magharibi cha dunia, ambaye anajitambulisha Mwenyewe kati ya kanisa usiku huu, Yeye yule jana, leo, na hata milele. Ile Nuru ya jioni ya Mwana imekuja. Leo Maandiko haya yametimia mbele yetu.

JE! TUKO KATIKA MAPENZI MAKAMILIFU YA MUNGU KWA SISI KUSEMA NA KUAMINI KUWA: “KUZICHEZA KANDA NDIO NJIA ILIYOANDALIWA NA MUNGU KWA AJILI YA BIBI-ARUSI WAKE”?

JE! KUNA KITU KILICHO KIKUU ZAIDI YA KUZISIKILIZA KANDA?

Kila mara katika utatu kama nilivyosema usiku uliopita Mungu huwakilishwa. Pale kulikuwako Wasodoma. Walutu, na Waibrahimu. Ni hali ile ile usiku huu, ulimwengu ukikaa tu hivyo!
Tazama, Yule aliyekaa pamoja na Ibrahimu alikuwa Mungu Mwenyewe; na wale wengine wawili walikuwa Malaika wajumbe.

KWA HIVYO NI NANI ANAYEZUNGUMZA NASI KWENYE KANDA?

Hebu niwaulizeni kitu fulani. Tazama utaratibu huu sasa. Ibrahimu alimwita huyu aliyeongea naye, “Elohim.” Neno la Kiebrania Elohim maana yake ni “Yule aridhishaye kwa vyote. Yeye yule Aliye wa Milele,” Elohim, Mungu Mwenyewe!

NI MUHIMU JINSI GANI KUBONYEZA PLAY?

…“wakati mmoja Roho Mtakatifu atakuja na kufanya mambo yale yale, na kunena tu neno moja dhidi Yake hautasamehewa kamwe. Hiyo ni siku hizi, ambapo kila neno yapasa liunganike pamoja. Nena neno dhidi Yake, halitasamehewa katika dunia hii wala dunia ijayo.”

Haleluya zetu za wiki iliyopita na kumsifu Bwana zilikuwa ni maandalizi tu ya kutuandaa kwa ajili ya kile kitakachotendeka Jumapili hii, Kwani Bibi-arusi kwa mara nyingine tena anaungana na kumsikiliza MUNGU akitutia moyo na kutuhakikishia kwamba sisi ndiyo wateule Wake, Naye anakuja hivi karibuni kutupeleka kwenda kwenye Karamu yetu kuu ya Harusi, kisha Makao yetu ya Baadaye.

Siku hii ndiyo aliyoifanya BWANA; tutashangilia na kuifurahia.

Ndugu Joseph Branham

Ujumbe: 65-0219 – “Leo Maandiko Haya Yametimia”

Maandiko:
Yohana Sura ya 16
Isaya 61:1-2
Luka 4:16

26-0301 Ile Mbegu Haitarithi Pamoja Na Kapi

UJUMBE: 65-0218 Ile Mbegu Haitarithi Pamoja Na Kapi

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi Neno Bikira,

Nimeketi hapa asubuhi ya leo nikiuhisi upako Wa aina yake ninapousikiliza, kuusoma na kujifunza Ujumbe huu ambao Bibi-arusi atakaousikia Jumapili. Utu wangu wote umejaa upako. Moyo wangu unabubujika kwa furaha kubwa nikijua, SOTE TUTAKUSANYIKA PAMOJA KUTOKA KOTE ULIMWENGUNI KWA UPAKO HUU ULE ULE. Tutakuwa tukifurahi, tukimsifu Bwana, sote kwa wakati mmoja, Yeye anapozungumza na kila mmoja wetu na kulifunua Neno Lake.

Upako utakuwa mkubwa sana hivi kwamba kutakuwa na kupiga makelele na kupaza sauti, “haleluya, amina, Jina la Bwana lisifiwe” kote ulimwenguni kwa wakati mmoja, tunapovumisha Mbingu kwa sifa na kuabudu kwetu.

Kitu gani kitakachotukia? Mungu atakuwa akimuunganisha na kuzungumza na Bibi-arusi Wake. Tutakuwa Jamii Moja, katika nia moja kwa umoja anapojifunua na kujidhihirisha Mwenyewe kwetu.

Hakuna mahali pakuu zaidi unapoweza kwenda, hakuna Sauti kuu zaidi unayoweza kuisikia; hakuna upako mkuu zaidi kuliko Sauti ya Mungu ikizungumza nawe moja kwa moja kwenye kanda.

Mungu amelilinda Neno Lake tangu mwanzo na ameandaa mahali ambapo watoto Wake wote wanaweza kwenda na kumsikia Yeye akinena na kulifasiri Neno Lake Mwenyewe. Mahali ambapo hakuna kubahatisha, hakuna kutumai, hakuna kushangaa-shangaa; Ndio mahali palipoandaliwa na Mungu pa kuisikia BWANA ASEMA HIVI.

Wakati hilo linapofunuliwa kwako, ni kama nuru kubwa ambayo imewashwa moyoni na nafsini mwako…unapaza sauti, “hili ndilo. Naliona. Mimi ni MMOJA NA NENO. MIMI NI NENO. MIMI NDIYE BIBI-ARUSI. NIMEWASILI.”

Linatendeka, nao hawajui. Hiyo ni kweli. Mwaona? Naam, bwana! “Kwa kuwa po pote ulipo mzoga, ndipo watakapokusanyika tai,” halisi tu kama ulimwengu. Unaona? Hivyo ndivyo ilivyosema. Je, mzoga ni nini? Neno. Yeye ni Neno, mzoga, Kristo! “Kristo ndani yako” yeye yule jana leo, na hata milele. Jinsi ilivyo kweli!

Tunapokusanyika kulisikiliza Neno, wasiwasi wetu wote, msongo wetu wote wa mawazo, matatizo yetu yote, hutoweka tu. Tunafurahi tunapogundua kuwa hatuna cha kuwa na wasiwasi nacho; sisi ni Bibi-arusi Wake. Yeye Hayuko tu pamoja nasi, BALI YU NDANI YETU. SISI NI ILE MBEGU BIBI-ARUSI NENO. Kila kitu ni kikamilifu. Wakati Wake ni mkamilifu. Sisi ni wakamilifu.

Tumeridhika mno na kushukuru sana kusema sisi ni Neno Lake lililodhihirishwa tuliyozaliwa kibikira; Yesu Kristo yeye yule jana, leo, na hata milele, akiishi na kukaa ndani yetu. Haleluya!

Hatuwezi kupatana hata kwenye NENO MOJA. Lazima tuisikie Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda.

Je, umepata kuona tai akipatana? La, bwana! Yeye hapatani kamwe. Wala Mkristo halisi pia. Yeye si mtu mdhaifu. Yeye atawinda hata atakapoipata. Amina! Naam, bwana! atapata nyama yake. Yeye anataka mana mpya. Atafika kule na kuchimbua mpaka aipate. Ataruka juu zaidi na zaidi. Iwapo haimo kwenye bonde hili, ataruka juu zaidi. Kadiri urukavyo juu, ndivyo unavyoweza kuona mbali zaidi. Kwa hivyo ni wakati wa tai wa siku hizi kuruka juu zaidi, wakachimbue kwenye ahadi za Mungu, si kuishi kwa chakula cha mwewe kilichouawa miaka mingi iliyopita. Tokeni kwake.

Kaa tayari ewe Bibi-arusi, tutaila Mana hiyo mpya, tukiketi chini ya ule upako mkuu zaidi uliopo, Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(Ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) tunaposikia: 65-0218 Ile Mbegu Haitarithi Pamoja na Kapi.

Tunawaalika Bibi-arusi kutoka kote ulimwenguni kuungana nasi kula kwenye Njia kamilifu ya Mungu iliyoandaliwa kwa ajili ya siku hii. Mahali pekee ambapo BIBI-ARUSI Anaweza kusema amina kwa kila Neno. Ambapo upako mkuu wa Roho Mtakatifu unaponena na kumkamilisha Bibi-arusi Wake kwa Kubonyeza Play na kusikia na kulipokea Neno Lake.

Ndugu. Joseph Branham

Maandiko:
Mathayo 24:24
Luka 17:30
Yohana 5:24 / 14:12
Warumi 8:1
Wagalatia 4: 27-31
Waebrania 13:8
1 Yohana 5:7
Ufunuo 10
Malaki 4

26-0222 Mtu Anayejiepusha Na Uso Wa Bwana

UJUMBE: 65-0217 Mtu Anayejiepusha Na Uso Wa Bwana

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wana-kondoo,

Ni heshima na majaliwa yaliyoje kusema, “Sisi ni wana-kondoo wa Mungu, ambao Yeye alimtuma malaika-mjumbe Wake wa saba kuwaita na kuwalisha Mana Yake iliyohifadhiwa na iliyofichwa.”

Tumeridhika na tunaamini Ujumbe huu ni Sauti ya Mungu ambayo imetumwa kumkamilisha Bibi-arusi Wake. Tunaamini kapi linajiondoa kwenye ngano, na sasa Bibi-arusi Wake amekaa katika Uwepo wa Mwana, AKIBONYEZA PLAY apate kuiva.

Na hilo ndilo kusudi letu la kuwa hapa, rafiki, kukaa katika Uwepo wa Mwana hata kundi letu dogo la watu hapa, hata litakapoiva sana kwa ajili ya Kristo, liwe mkate kwenye meza Yake. Hivyo ndivyo ninalitaka lifanye.

Yeyote ambaye haamini kwamba KUBONYEZA PLAY na kuisikia Sauti ya Mungu iliyothibitishwa ikinena ndiyo Sauti iliyo muhimu zaidi unayopaswa kuisikia, ni mtu anayejiepusha na uso wa Bwana.

Hamna budi kulikabili, ama kufanya jambo fulani juu yake.Una jukumu, kila mtu analo, nawe huna budi kukabiliana na mambo haya.

Jinsi gani nukuu hii ilivyo ya kweli na muhimu kwa ajili ya siku hii. Kuna mgawanyiko mwingi miongoni mwa walioitwa watoke wa Mungu. Je, ni muhimu zaidi kuzicheza kanda kanisani ili kuisikia Sauti ya Mungu, au hivi sasa ni muhimu zaidi wahudumu kulihudumu Neno?

Mungu amewaita na kuwaweka wahudumu hapa ili kulidumisha Neno mbele ya watu. Wao ni Wachungaji. Neno linafundisha hili. Wanapaswa kuheshimiwa na kutambuliwa kama watu ambao Mungu amewaita na kuwaweka.

Hatuwezi, na hatupaswi, kusema kamwe wao si Bibi-arusi. Hilo ni KOSA na si kulingana na kile nabii alichotufundisha. Nimesikia watu wakisema: “Kama hawachezi kanda makanisani mwao, wao ni wapinga Neno.” Haupaswi kamwe kusema kitu kama hicho. Hilo linanionyesha una roho asiye sahihi.

Nimesikia wengine wakisema, “Wote lazima wasikilize hewani pamoja na BT la sivyo wako nje ya mapenzi ya Mungu”. Haupaswi kamwe kusema kitu kama hicho. Mungu peke yake ndiye anayejua ni nani aliye Bibi-arusi na ni nani asiye. Hiyo si roho ya Bibi-arusi kusema kitu kama hicho.

Hata baadhi ya watu wanaosikiliza hewani pamoja na BT wanasema, “ukienda kanisani kusikiliza kanda na usisikilize hewani nyumbani mwako umekosea!” Hilo si sahihi ndugu na dada. Kama unasema hivyo, ACHA, umekosea. Kila mmoja lazima wafanye vile WANAVYOJISIKIA WANAONGOZWA NA BWANA KUFANYA.

Wahudumu wengi wanahisi kuhubiri ndio njia iliyoandaliwa na Mungu kwa ajili ya siku hii. Sisi tunaona tu mambo tofauti, hiyo ni sawa. Ni mara ngapi Ndugu Branham alifanya ulinganisho huu uleule? Tumetoka kumsikia kwenye Maswali na Majibu, watu walipokuwa wakizungumza kuhusu Ndugu Jackson kuwa amekosea, aliwakemea kusema lolote dhidi yake na kanisa lake.

Mimi ndo nahubiri hivyo kwa njia ya barua hii kile Mimi ninachoamini ndio njia iliyoandaliwa na Mungu kwa ajili ya Maskani ya Branham. Wao ni ndugu na dada zetu. Wanampenda Bwana na Ujumbe huu. Hivyo ndivyo wanavyohisi Bwana anawaongoza. Bwana asifiwe.

Wao wanaliona kwa njia moja na sisi tunaliona kwa njia nyingine, hilo ni sawa. Mimi siwezi kuliona kwa njia yao nao hawawezi kuona yangu. Nionavyo mimi, kuna njia nyingi ambazo Mungu ameandaa, lakini kuna NJIA MOJA TU KAMILIFU, NA KWANGU MIMI, HIYO NI KUBONYEZA PLAY.

Natumai sieleweki vibaya hapa. Kuweka mikono na kuwaombea watu ni 100% kulingana na Neno. Kupakwa mafuta na kuwaombea wagonjwa ni Neno la Mungu kulingana na Maandiko. Ndugu Branham alituhubiria na kutufundisha yote kuwa ni Neno. Lakini Mimi naitaka NJIA KAMILIFU YA MUNGU ALIYOIANDAA….KUAMINI TU KWA SABABU MUNGU ALISEMA HIVYO. Hilo ndilo ninalojitahidi kufanya.

Lakini sasa kwa ajili ya uponyaji, ni rehema ya Mungu tu kwamba Yeye, “Kwa kupigwa Kwake wewe uliponywa.” Sasa, kwanza Neno linasema hivyo, linapaswa kutosha, lakini ikiwa huliamini katika Neno, basi kuna karama Kanisani, kama vile wanaume waliovuviwa kujua jinsi ya kufundisha hilo, hilo litalifanya liwe wazi kwako, ndilo, na imani ya kuamini.

Ninaamini katika huduma 5. Ninaamini katika watu walioitwa na Mungu kuhubiri na kulifundisha Neno. Lakini, naamini kuisikia Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda ndio NJIA KAMILIFU YA Mungu KWANGU MIMI.

Katika kuzisikiliza kanda, sihitaji hata kuelewa, NAAMINI TU KILA NENO NINALOSIKIA. Hakuna mtu, hakuna mhudumu, hakuna mahali pengine ninapoweza kwenda ambapo ninaamini KILA NENO na kukiweka kikomo changu cha Milele, isipokuwa kanda.

Haijawahi kutokea tangu mwanzo wa wakati Mungu kuwapa watu Wake fursa na uwezo wa kuisikia Sauti Yake wao wenyewe ikizungumza mdomo kwa sikio. Kila siri inafunuliwa kwenye kanda. Kila swali linajibiwa kwenye kanda. Kila kitu Bibi-arusi anachokihitaji ili kukamilishwa kiko kwenye kanda.

Kila Neno lililonenwa kwenye kanda ni Neno la Mungu. Huenda nisielewe ama nisiweze kuelezea kila kitu, lakini si lazima nifanye hivyo. Yeye ananitaka tu niseme AMINA KWA KILA NENO, nazo KANDA ndio mahali PEKEE ninapoweza kufanya hivyo.

Bali inapo—inapokulazimu kufanya jambo ambalo ni tofauti, wakati inapokulazimu kutetea unayoamini kuwa ni Kweli, hiyo ndiyo sehemu iliyo ngumu, hapo ndipo mkwaruzo unapokuja, papo hapo.

Ninaamini kwa yote yaliyo ndani yangu, tuko katika Mapenzi makamilifu ya Mungu na katika meli inayoelekea Ninawi. Ningependa ulimwengu wote uje usafiri pamoja nasi katika meli yetu Jumapili hii saa 6:00 MCHANA,. Masaa ya Jeffersonville,(Ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) tunapomsikia Mungu akizungumza na Wana-kondoo Wake.

Ndugu. Joseph Branham

Ujumbe: 65-0217 “Mtu Anayejiepusha Na Uso Wa Bwana”

Maandiko ya kusoma:
Yona 1:1-3
Malaki 4
Yohana Mtakatifu 14:12
Luka 17:30

26-0215 Maswali na Majibu #4

UJUMBE: 64-0830E Maswali na Majibu #4

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Familia ya Kifalme,

Kuna mahali PAMOJA tu palipothibitishwa ambapo unaweza kwenda kumsikia Bwana akinena kupitia malaika Wake na kukuambia, “Daima Kumbukeni, ninyi ni watoto wa Mungu, Familia ya Kifalme wenye Damu ya Kifalme. Hakuna Damu bora zaidi duniani kuliko yenu. Ninyi ni watoto wangu, mmetawanyika kote ulimwenguni, ambao nimemzalia Kristo.”

Sisi ni Familia ya Mungu ya Kifalme wenye Damu ya Kifalme ikitiririka mishipani mwetu. Watoto aliomzalia Kristo kwa Sauti ya Mungu inenayo kupitia nabii Wake mwenye nguvu. Hakuna njia bora ya kulieleza kuliko hiyo, enyi marafiki.

Ndugu Branham, je, Bibi-arusi atahitaji kuhamia Jeffersonville au Arizona ili kuwa katika Unyakuo?

“Wawili watakuwa kitandani; nitamtwaa mmoja na kumwacha mmoja; na wawili watakuwa kondeni; nitamtwaa mmoja na kumwacha mmoja.” Ona? Kwa hivyo huenda wao…Kote ulimwenguni, hawatakusanyika mahali pamoja na kuwa na vitu shirika. Lakini makundi madogo yatakuwa yametawanyika kote duniani.

Kwa hivyo kimwili, hatutakuwa mahali pamoja kwa wakati mmoja. Bali utukufu kwa Mungu, Yeye alikuwa na mpango mkuu zaidi wa kumkusanya Bibi-arusi Wake pamoja.

Tunayaombea makanisa yote na makusanyiko ambayo yamekusanyika kuzunguka vile—vile—vile vipaza sauti vidogo nchini kote, kutoka kwenye taifa, kote kote hata kwenye Pwani ya Magharibi, kule juu kwenye milima ya Arizona, chini kwenye mabonde ya Texas, mbali sana hata Pwani ya Mashariki, nchini kote, Bwana, ambako wao wamekutanika. Tuko umbali wa masaa mengi, bali, Bwana, sisi tuko pamoja usiku wa leo kama jamii moja, waamini, tukingojea kuja kwa Masihi.

Leo, si tu kwamba Yeye anamkusanya Bibi-arusi Wake kutoka kote nchini, bali pia Yeye anatukusanya SISI kutoka mabara 7 ya dunia. Kuanzia Afrika hadi Antaktika. Amerika Kaskazini hadi Amerika Kusini, Asia, Australia na Ulaya. Yeye anamkusanya na kumuunganisha Bibi-arusi Wake kama JAMII MOJA ili kuisikia Sauti ya Mungu.

Yeye alituambia twende kanisani; hata pale wafundishapo nusu ya Neno, MPAKA tutakapolipata kanisa ambapo wanafundisha NENO LOTE. Mungu asifiwe Bibi-arusi Sasa yeye amepapata mahali hapo, ni Sauti ya Mungu iliyo kwenye Kanda ndio NENO LOTE.

Iwe uko katika kanisa lako la Kanda la Nyumbani, kanisa lako ambamo familia nyingi zimekusanyika, au katika kibanda katika misitu ya Amazon au Afrika, popote unapoweza Kubonyeza Play kuisikia Sauti ya Mungu ikizungumza nawe mdomo kwa sikio, utakuwa u katika KANISA LA NENO LOTE.

Sisi tumelipata hilo kanisa la Neno lote nasi tunakualika uungane nasi Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(Ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) tunaposikia: Maswali na Majibu #4 64-0830E.

Ndugu Joseph Branham

26-0208 Maswali na Majibu #3

UJUMBE: 64-0830M Maswali na Majibu #3

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Aliomzalia Kristo,

Mtu anawezaje kuuweka katika maneno matupu ya kibinadamu upendo na furaha iliyo mioyoni mwetu kuujua Ufunuo wa kweli wa Neno Lake kwa ajili ya siku yetu? Kuwazia, hatukuwa na uhusiano wowote nalo, lakini YEYE, Yule MIMI NIKO aliye Mkuu, kwa uchaguzi Wake Mwenyewe, Yeye alituchagua SISI kimbele kuwa na kitu kikubwa zaidi ambacho angeweza kutupa, UFUNUO WA NENO LAKE KWA AJILI YA WAKATI WETU.

Yeye alingoja, hadi utimilifu wa wakati ulipotimia, atupulizie pumzi ya uhai ndani yetu, ili tuweze kumsikia Yeye akizungumza nasi na kusema:

Sasa, nimejaribu kadiri niwezavyo ku—ku—kuwaarifu ninyi watu na kuwaongoza kama baba angewaongoza watoto wake. Ninyi mu watoto wangu; nimewazaa katika Kristo kwa Injili hii ninayohubiri. Ona? Nami—ni—ni—ninawatakeni mkuze watoto waliokomaa vilivyo, au—au watoto. Nami nataka kuwakabidhini Kristo siku hiyo, kama vile Paulo alivyosema, “Bikira safi.” Hakuna kitu katika Neno ila lile moyo wako utaitikia kwa “amina.”

Mungu, akinena kupitia malaika Wake mwenye nguvu, anatuelekeza na kutuongoza, Bibi-arusi wa Yesu Kristo. Sisi ndio bikira Wake safi, watoto waliyokomaa. Na kwa neema Yake ya ajabu, tunaliitikia kila Neno tunalosikia kwa AMINA! Ndio fasiri kamilifu ya Neno lenye thibitisho la Kiungu!

• Ikiwa Sauti tunayoisikia kwenye kanda ndio: fasiri kamilifu ya Neno, ni kitu gani kingine ambacho Bibi-arusi wa Yesu Kristo anachohitaji?… HAKUNA!

Yeye ametuchagua SISI, kundi Lake dogo alilolichagua kwa mkono Wake, ili tuwe na Ufunuo wa kweli wa Neno Lake la wakati wetu. Sisi ndio aliowachagua kuwapo duniani, katika miili ya nyama, wakati wa ile miaka elfu moja ya Utawala wa Miaka Elfu.

Enyi marafiki, hebu tulizungumzie hilo kwa dakika moja.

Tutakuwa na mwili uliotukuzwa papa hapa duniani. Tutakuwa tukila, tukinywa, tukijenga majumba, tukiishi kama tunavyoishi sasa kwa miaka elfu moja. Itakuwa ni fungate yetu ambapo Bibi-arusi (SISI) na Bwana harusi (Bwana Yesu Kristo) wamefanyika MMOJA.

Tunakesha na kungoja wakati huu mtukufu kila dakika ya kila siku. Uko karibu sana kiasi kwamba inaonekana kama tunaweza kuugusa. Ninaamini, kwa moyo wangu wote, hili ndilo linalotendeka kwetu sisi leo:

Loo, huo muungano wa kiroho wa Kristo na Kanisa Lake sasa, wakati mwili unapofanyika Neno, nalo Neno linafanyika mwili, linadhihirishwa, linathibitishwa. Vile vile hasa Biblia ilivyosema ingetendeka katika siku hii, inatendeka, siku baada ya siku. Mbona, inalundikana upesi sana huko nje, katika yale majangwa, na mambo yanayotendeka, hata nisingeweza kufuatilia jambo hilo. Tuko karibu na kule Kuja kwa Yesu, kuunganishwa na Kanisa Lake, ambapo Neno linafanyika Neno.

Kwa kila Ujumbe tunaosikia, ndivyo Yeye anavyozidi kutupata Ufunuo zaidi. Unalundikana upesi sana hivi kwamba hata hatuwezi kufuatilia jambo hilo. Tunaliona Neno likifanyika Neno zaidi ya wakati wowote. Hakuna shaka moja hata chembe; kwa Ufunuo, tunajua sisi ni nani haswa.

Yeye anamuunganisha Bibi-arusi Wake kama vile tu alivyosema angefanya, nasi tu sehemu ya hilo. Tunaliona likitendeka kwa macho yetu wenyewe. Wengine huenda wasilione ama kulielewa. Hilo si kwa ajili yao, NI KWA AJILI YETU SISI, WATOTO WAKE ALIOWAZAA.

Bibi-arusi walikuwa na maswali ya kumuuliza nabii.

Je, inatosha kusikiliza Sauti ya Mungu PEKE YAKE kwenye kanda? Mungu alijibu na kusema: NDIYO!!

Je, watoto wetu pia wanaweza kupata kila kitu wanachokihitaji ili kuwa Bibi-arusi wa Kristo kwa kusikiliza kanda tu: NDIYO!!

Kwa hivyo, Kila kitu Bibi-arusi anachokihitaji kipo KWENYE KANDA.

Pia tunajua Mungu ameziandaa njia zingine nyingi kwa ajili ya watoto Wake.

“Kwa kupigwa Kwake wewe uliponywa.” Sasa, kwanza Neno linasema hivyo, hilo linapaswa kutosha, lakini ikiwa huliamini katika Neno, basi kuna karama Kanisani, kama vile wanaume waliovuviwa kujua jinsi ya kufundisha hilo, hilo litafanya liwe wazi kwako, ndilo, na imani ya kuamini.

Tunashukuru mno Mungu amewaandaa wanaume waliovuviwa kujua jinsi ya kufundisha uponyaji na Neno Lake ili kulifanya wazi kwa wengine, lakini Bibi-arusi Wake anataka NJIA YAKE KAMILIFU ILIYOANDALIWA ITOSHELEZAYO. Ndiyo tu TUNAYOHITAJI.

Ningependa kuwaalika muungane na Maskani ya Branham Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(Ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) tunaposikia: Maswali na Majibu #3 64-0830M.

Ni jambo la kupendeza vipi kuwa na Ufunuo wa Neno Lake na kujua kwamba sisi ni Neno lililofanyika mwili.

Ndugu Joseph Branham

26-0201 Maswali na Majibu #2

UJUMBE: 64-0823E Maswali na Majibu #2

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wana Tai,

Palipo na Mzoga, hapo ndipo Bibi-arusi watakapokusanyika. Na kwetu sisi, kuna mahali pamoja tu pa kamilifu tunapoweza kuipata hiyo nyama mbichi ya Mana: kwa kubonyeza play na kuisikia Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda.

Nena kuhusu Mana MPYA, Je, hivi tunaweza hata kuanza kuwazia kile tulicho nacho katika ncha ya vidole vyetu? Sauti halisi ya Mungu ikizungumza na Bibi-arusi Wake mpendwa kwenye kanda, ambapo hakuna kubahatisha, hakuna kushangaa, hakuna kuhoji wala kutilia shaka kile tunachokisikia ni Mungu, akitumia sauti ya mwanadamu, kunena Bwana Asema Hivi kwa Bibi-arusi Wake.

Kwa ufunuo, tunaamini ndipo mahali PEKEE tunapoweza kwenda na kuzipumzisha nafsi zetu kwamba Maneno tunayoyasikia si neno la mwanadamu, wala fasiri yake au wazo lake halijaongezwa Kwake, bali ni Neno safi la Mungu likizungumza nasi wana tai, akilifunua Neno Lake.

Tunashiriki kwenye Neno. Tunalisoma Neno Lake katika Biblia zetu.  Hata tunawasikia watu waliyowekwa wakfu na kuitwa waliojazwa na Roho Wake Mtakatifu, wakilinukuu na kulihubiri Neno la Mungu, bali katika wakati wetu, Mungu ameandaa mahali ambapo sisi tunaweza kulisikia NENO Lake KAMILIFU LIKINENWA, kwa kubonyeza Play.

Baba hata Yeye anampa Bibi-arusi Wake fursa ya kuuliza maswali yaliyokuwa mioyoni mwetu ili tupate jibu lililo kamilifu:

  • Je, Shetani anaweza kutumia karama za lugha au ya unabii katika mtu aliye na Roho Mtakatifu?
  • Yesu alimaanisha nini katika Mathayo 12, mstari wa 32?
  • Tafadhali fafanua Wakorintho wa Kwanza 13:8-12.
  • Je, wanawake wanaruhusiwa kufanya kazi katika mahali pa umma hali wakiwa na waume wenye afya na watoto?
  • Je, ni kosa kwa mwanamke kusokota nywele zake?

Mungu ameandaa njia nyingi sana za kumbariki na kumtia nguvu Bibi-arusi Wake, lakini kuna mahali pamoja tu Yeye alipopaandaa ambapo Bibi-arusi Wake wanaweza kuwa na ujasiri 100% kuwa kile wanachokisikia ni NENO LAKE KAMILIFU. Chemchemi Moja ya Maji ya Uzima ambapo Wana tai wanapoweza kunywa ambapo hakuna uwezekano wa vimelea vyovyote. BONYEZA PLAY.

Ninakualika uje kunywa kutoka kwenye Chemchemi hiyo Jumapili hii saa 6:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(Ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) ambapo tutasikia 64-0823E “Maswali na Majibu #2.”

Ndugu Joseph Branham

26-0125 Maswali na Majibu #1

UJUMBE: 64-0823M Maswali na Majibu #1

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Maskani Ya Branham,

Salamu kwa Bibi-arusi wa Yesu Kristo waliopo kote ulimwenguni, wanaoamini Maskani ya Branham, Sauti ya Mungu, ndio kanisa lao la nyumbani ambapo wanalishwa kiroho kwa Mana iliyofichwa ambayo imehifadhiwa na kutunzwa kwa ajili ya Bibi-arusi wa Kristo.

Hiki ndicho kituo changu cha nyumbani; haya ndiyo makao yangu makuu; hapa ndipo tumeimarika. Sasa, shikilia hilo mawazoni haijalishi itakuwaje. Sasa, kama mna busara, mtashika jambo fulani. Haijalishi itakuwaje, haya ndiyo makao yetu makuu, papa hapa!

Waamini wengi wamekuwa wakielewa vibaya au kuweka wazo lao wenyewe au fasiri yao wenyewe kwenye kile nabii alichosema hapa, bali yeye anamwambia Bibi-arusi moja kwa moja, “kama mna busara, mtashika jambo fulani, haya ndiyo makao yetu makuu, papa hapa!”

Alimaanisha nini kwa jambo hilo?

Ndugu Branham alipokuwa hapa, wengi hawakumwelewa nao walidhani Bibi-arusi alipaswa kwenda Arizona na kumfuata yeye huko, ili waweze Kunyakuliwa. Ndugu Branham aliwajibu waziwazi: KAENI HAPA, HAPA NDIPO MAHALI PENYEWE.

Kundi kubwa mno lao waliondoka hivyo, nao walitaka kuenda hivi na kufanya yale baada ya mimi kuwaambia wakae pale. Kaeni pale, kaeni papa hapa; hapa ndipo mahali panapofaa.

Watu waliondoka kutoka kila mahali kote Marekani kwenda Arizona, lakini yeye aliwaambia waziwazi: Kaeni papa hapa, hapa ndipo mahali penyewe!

Kaeni Jeffersonville? Hivyo ndivyo yeye alivyosema!

Ufunuo wangu ni kwamba, ilikuwa ni Mungu, akizungumza kupitia nabii Wake na kuwaambia watu, “KAENI NA KANDA.” Hapo ndipo MAHALI PENYEWE!

Alikasirika mno na akasema ilibidi afanye jambo fulani kuhusu watu hao wote. Yamlazimu afanye nini? Angewapeleka kwenye kanisa gani? Wao wanapaswa waende wapi? Ndugu Branham alisema inamlazimu afanye nini?

Kwa hivyo sasa, yanipasa kuwarudisha hao watoto hapa wapate kula. Wako chini kule jangwani wakiumia kwa njaa.

Yeye hakusema ati wangehitaji kwenda kwenye kanisa la mahali na kupata vipande vidogo ambavyo wangeweza kula. Yeye alisema lazima AWARUDISHE HAPA wapate kula, la sivyo WANGEKUFA KWA NJAA.

UFUNUO WANGU, Enyi MARAFIKI.

Sasa, msimwelewe vibaya kwa mara nyingine tena, au kusema kitu fulani ambacho hakusema, kwa kusema, “Ndugu Branham alitaka kila mwamini ahamie Jeffersonville ili kuwa Bibi-arusi.” Ndugu Branham aliwajua watu hao wote, na KILA mwamini kutoka kote ulimwenguni, hawangeweza kuhamia na kuishi Jeffersonville. Hilo lisingewezekana. Kwa hivyo yeye alimaanisha nini? Yeye alikuwa ANAMUUNGANISHA Bibi-arusi wa Kristo kwenye KANDA ambazo zilikuwa zimerekodiwa na kuhifadhiwa kwa ajili ya Bibi-arusi kuzila.

Ujumbe huu, Sauti Hii, ndilo Neno la Mungu Lililonenwa kwa ajili ya siku hii nalo Litamuunganisha na kumkamilisha Bibi-arusi wa Yesu Kristo.

Mzoga ni kile anachokula tai. Sasa, tai huhesabiwa katika Biblia, nabii. Nabii ni tai. Mungu—Mungu hujiita Mwenyewe Tai, nasi tu “wana tai” basi, wa—waamini. Mwaona? Na mzoga waulao ni nini? Ni Neno. Po pote lilipo Neno, tabia halisi ya ndege itajidhihirisha yenyewe.

Liko wapi Neno la Bwana lililo safi, lililothibitishwa, lisilo na mkanganyiko, Bwana Asema Hivi kwa ajili ya siku hii? Kuna mahali pamoja tu, kwenye Kanda.

Ningeweza kuendelea na kuendelea, nukuu kwa nukuu, lakini Ujumbe huu na kile Ndugu Branham alichosema kinahitaji Ufunuo kutoka kwa Mungu. Yatupasa kusoma katikati ya mistari kwa ufunuo, bali tuseme kile yeye alichosema. Kwa maana ni NENO SAFI.

Maswali na Majibu ya leo na kile MIMI NINACHOAMINI.

Leo, wahudumu wengi wanawaambia watu kwamba kwa sisi kuwa na Kanisa La Kanda La Nyumbani tumetoka nje ya Neno na kile Ndugu Branham alichosema tufanye. Wao wanahisi ni lazima tuende kwenye kile wanachokiita na kukichukulia kanisa.

Kuna nukuu nyingi, nyingi sana kiukweli ambapo Ndugu Branham analisema hili waziwazi.

Sasa, ninyi endeni kwa kanisa fulani nzuri la Injili Nzima mpate kanisa la nyumbani.

Nami naliamini hilo kwa moyo wangu wote, kwa sababu yeye alisema hivyo. Lakini naamini sisi tunafanya hivyo kwa KUWA NA KANISA LA KANDA LA NYUMBANI. Mahali petu si ndipo palipo muhimu kwa Bwana. Hilo ni jengo tu. Lakini wajibu wetu kwa Bwana ni kukaa na Neno Lake, SIO MAHALI AU JENGO. Mahali hapo hapamwokoi na kumkamilisha Bibi-arusi, NENO NDILO.

Kama nikienda kwenye jengo la kanisa, lakini wao wamesahau JAMBO LILILO KUU: kuisikia Sauti ya Mungu kwa Kubonyeza Play, nao wameibadilisha hiyo kwa kuwasikia wahudumu TU wakiuhubiri Ujumbe, Je, hilo litairidhisha na kuilisha nafsi yako kabisa? Huenda hilo likairidhisha nafsi yako, ndugu na dada yangu, bali hilo halitamridhisha Bibi-arusi.

Hebu niingilie kati hapa na niseme kuna maelfu ya watu ambao hawana jengo la kanisa la kwenda. Je, wamepotea? Ikiwa hawana mchungaji au kanisa, Je, hiyo ina maana kwamba hawawezi kuwa Bibi-arusi? Ikiwa unaishi ndani ya maili 100 kutoka kwenye jengo la kanisa, Je, ni lazima uende kwenye kanisa hilo? Lakini ikiwa ninaishi mbali zaidi, si lazima? Nalazimika kumsikiliza Mhubiri hewani, lakini siwezi kusikiliza kanda hewani? Je, jengo la kawaida ndilo ambalo nabii anasema ndilo jambo lililo muhimu zaidi tunalopaswa kwenda?

Nabii alitaka kumleta Bibi-arusi wapi?

Kama hamwezi kuja hapa maskanini, tafuteni kanisa fulani mahali fulani; enendeni kwalo.

Kwa mara nyingine tena, liko wapi chaguo lake la kwanza la kuwapeleka watu? Kwenye Maskani ya Branham, Neno, kanda. Hilo ndilo Mungu amempa Bibi-arusi Wake kufanya katika wakati huu wa mwisho, nasi tunafanya hivyo kila siku NA kila Jumapili.

Msinielewe vibaya. MIMI SISEMI lazima usikilize kanda hewani pamoja na Maskani ya Branham ili uwe Bibi-arusi. SISEMI hupaswi kwenda kanisani. SISEMI huwezi kuwasikiliza wahudumu. Ikiwa unaamini hivyo, uko nje ya Neno. Ninasema kuisikia Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda ndio Sauti iliyo muhimu zaidi UNAYOPASWA KUISIKIA, na ninaamini kwamba kila mchungaji anapaswa kuicheza Sauti hiyo, Kanda, katika makanisa yao. Lakini wao wametoa kila namna ya udhuru uliopo ILI KUTOZICHEZA KANDA. Ikiwa hilo ndilo kanisa lako, wewe huli Neno.

Hili ni wazi jambo ambalo yeye hakutaka litokee na ndicho ambacho watu walichokuwa wakifanya.

Nanyi nendeni kanisani; msiketi nyumbani, kuenda kuvua samaki, na kuwinda, na mambo kama hayo mnamo Jumapili.

Sisi hatufanyi hivyo. Sisi tunaungana kwenye kitu pekee kitakachomuunganisha Bibi-arusi, Ujumbe huu, Sauti hii.

Kwa mara nyingine tena, Mimi ninaamini katika kwenda kanisani. Kuna makanisa mengi ulimwenguni kote ambayo yanaziweka kanda nafasi ya kwanza kwenye mimbara zao, Bwana asifiwe. Je, ninaamini lazima ukae nyumbani la sivyo wewe si Bibi-arusi? LA, LA, LA….Sijawahi kuliwazia, sijawahi kuliamini. Nataka tu UBONYEZE PLAY bila kujali uko wapi au unaenda kwenye kanisa gani.

Kama huna Ufunuo wa kile anachosema, basi unaweza kusema waziwazi, “Sihitaji kumsikiliza Ndugu Branham au hata kulazimika KUKUBALIANA na yote asemayo. Hata hivyo alisema, kuna watu wengine wengi walioitwa na Mungu.”

Endelea. Twaona hapa lasema, “Yatupasa kuhuduria kanisa lingine lisilokubaliana nawe?” Hakika, si…Mimi siye changarawe pekee pwani, mwajua. Kuna—kuna watu wengine wacha Mungu kila mahali; natumai mimi ni mmojawao.

Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda ndio JIWE LA UFUKWENI LANGU, MWAMBA WANGU. Ndio Sauti ninayotaka Mimi kuisikia na ndio Sauti ninayotaka Maskani ya Branham waisikie.

Kama mngependa kuungana nasi, mnakaribishwa mno, ndugu na dada zangu. ungeneni nasi Jumapili saa 6:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) tunapoisikia Sauti ya Mungu ikinena na kuyajibu maswali mengi unayoweza kuwa nayo moyoni mwako. Na usikie mwenyewe ikiwa mambo niliyoyasema katika barua hii hayako sawa na Neno na nimeelewa vibaya kile Mungu anachomwambia Bibi-arusi Wake.

Kile yeye anachosema kwenye kanda ni Bwana Asema Hivi. Si kile mimi Ninachosema anasema, au kile Ninachoamini anasema, na Mungu PEKE YAKE ndiye anayeweza kukupa Ufunuo wa kweli.

Ndugu Joseph Branham

26-0118 Kuthibitisha Neno Lake

UJUMBE: 64-0816 Kuthibitisha Neno Lake

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi wa Kristo, hebu na tukusanyike pamoja Jumapili saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) kusikiliza 64-0816 – Kuthibitisha Neno Lake.

Ndugu Joseph Branham

26-0111 Makao Ya Baadaye Ya Bwana Arusi Wa Mbinguni Na Bibi-Arusi Wa Duniani

UJUMBE: 64-0802 Makao Ya Baadaye Ya Bwana Arusi Wa Mbinguni Na Bibi-Arusi Wa Duniani

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Kipenzi Cha Moyo Wangu,

Nakupenda sana. Wewe ni mwili wa mwili Wangu, na mfupa wa mfupa Wangu. Hata kabla sijaziumba nyota, mwezi, ulimwengu Wangu wote, nilikuona nami nilikupenda wakati huo. Nilijua wewe ulikuwa sehemu Yangu, Kipenzi Changu cha pekee. Wewe na Mimi tulikuwa MMOJA.

Ile siku ambayo nimeitamani na kuisubiri tangu nilipowaona hatimaye imefika. Sasa ninawaita na kuwaunganisha kutoka mashariki na magharibi, kaskazini na kusini, kwa Sauti Yangu. Ninyi ni mawazo Yangu, Neno Langu, Bibi-arusi Wangu, aliyedhihirishwa.

Nimetamani sana kuwaambia kila kitu kilicho moyoni Mwangu, kwa hivyo Nililiandika kupitia manabii Wangu na nimelilinda kwa maelfu ya miaka. Wengi wamelisoma, na kuliamini kwa karne nyingi, lakini nimeyaweka mambo mengi kuwa siri hadi NINYI MLIPOFIKA. Ninyi ndio WATU PEKEE nitakaowaambia.

Wao walitamani kuyajua na kuyasikia mambo haya yote ya ajabu ambayo nimeyaficha, lakini kama vile nilivyokuahidi, nimesubiri na kuyaweka kuwa siri hadi hivi sasa, kwa ajili yako WEWE tu, WANGU MMOJA NA WA PEKEE.

Nilikuahidi Mimi ningekuja na kujifunua Mwenyewe tena katika mwili wa mwanadamu, ili niweze kukuambia, na kukufunulia mambo haya yote. Nilitaka uisikie SAUTI YANGU ikizungumza nawe moja kwa moja.

Nimewatia mafuta wengine wengi kwa Roho Wangu Mtakatifu kukuambia kuhusu upendo Wangu, lakini kama nilivyofanya siku zote, Nami kamwe siwezi kubadilika, nilimchagua mtu mmoja: Malaika Wangu, Nabii Wangu, awe Sauti Yangu ili niweze kunena Bwana Asema Hivi kwako.

Nilitaka kukuambia, wewe hukuokolewa siku yoyote Maalum. Daima ulikuwa umeokolewa. Nilikuja tu kukukomboa. Uliokolewa tangu mwanzo kwa maana ulikuwa na Uzima wa Milele, kwanza. Kwa hivyo, machoni Pangu, dhambi zako zote haziwezi hata kuonekana Nami, kitu pekee ninachosikia ni sauti yako. Ninauona tu uwakilisho wako.

Jinsi gani nimesubiri kwa hamu kukuambia mambo mengi. Moyo wangu unabubujika kwa shauku. Jinsi gani nimeisubiri kwa hamu Karamu yetu ya Harusi, Miaka elfu moja ya Utawala wetu Wa Miaka Elfu tukiwa pamoja. Nikikuambia kwa undani kuhusu Makao Yetu ya Baadaye pamoja; Jinsi nilivyokuandalia kila kitu, kila kitu jinsi tu unavyopenda hasa.

Kipenzi Changu, ikiwa unaona ni vizuri mno sasa hivi kuisikiliza Sauti yangu ikizungumza nawe, subiri tu, hiki ni kivuli tu cha jinsi itakavyokuwa wakati tutakapoishi Katika ule Mji pamoja. Nabii wako yeye hata ataishi karibu nawe; atakuwa jirani yako.

Tutatembea kwenye barabara hizo za dhahabu na kunywa kutoka kwenye chemchemi pamoja. Tutatembea katika paradiso za Mungu huku Malaika wakiizunguka dunia, wakiimba nyimbo za sifa….Itakuwa ni Siku ya namna gani!

Najua njia inaonekana inaparuza, na wakati mwingine inakuwa ngumu kwako, lakini itakuwa kitu kidogo sana, kidogo sana, Tutakapokuwa pamoja.

Kwa sasa, nitakukusanya Kwa mara nyingine tena na kuzungumza nawe Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville, (ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) na kukuambia kila kitu kuhusu “Makao Ya Baadaye Ya Bwana Arusi wa Mbinguni na Bibi-arusi wa Duniani”. Nasubiri kwa hamu kuungana nawe wakati huo.

Kumbuka, na kamwe usisahau, nakupenda sana.

Kwa niaba Yake,

Ndugu Joseph Branham

Maandiko:
Mathayo Mt. 19:28
Yohana Mt. 14: 1-3
Waefeso 1:10
2 Petro 2:5-6 / Sura ya 3
Ufunuo 2:7 / 6:14 / 21:1-14
Walawi 23:36
Isaya Sura ya 4 / 28:10 / 65:17-25
Malaki 3:6