Category Archives: Uncategorized

26-0118 Kuthibitisha Neno Lake

UJUMBE: 64-0816 Kuthibitisha Neno Lake

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi wa Kristo, hebu na tukusanyike pamoja Jumapili saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) kusikiliza 64-0816 – Kuthibitisha Neno Lake.

Ndugu Joseph Branham

26-0111 Makao Ya Baadaye Ya Bwana Arusi Wa Mbinguni Na Bibi-Arusi Wa Duniani

UJUMBE: 64-0802 Makao Ya Baadaye Ya Bwana Arusi Wa Mbinguni Na Bibi-Arusi Wa Duniani

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Kipenzi Cha Moyo Wangu,

Nakupenda sana. Wewe ni mwili wa mwili Wangu, na mfupa wa mfupa Wangu. Hata kabla sijaziumba nyota, mwezi, ulimwengu Wangu wote, nilikuona nami nilikupenda wakati huo. Nilijua wewe ulikuwa sehemu Yangu, Kipenzi Changu cha pekee. Wewe na Mimi tulikuwa MMOJA.

Ile siku ambayo nimeitamani na kuisubiri tangu nilipowaona hatimaye imefika. Sasa ninawaita na kuwaunganisha kutoka mashariki na magharibi, kaskazini na kusini, kwa Sauti Yangu. Ninyi ni mawazo Yangu, Neno Langu, Bibi-arusi Wangu, aliyedhihirishwa.

Nimetamani sana kuwaambia kila kitu kilicho moyoni Mwangu, kwa hivyo Nililiandika kupitia manabii Wangu na nimelilinda kwa maelfu ya miaka. Wengi wamelisoma, na kuliamini kwa karne nyingi, lakini nimeyaweka mambo mengi kuwa siri hadi NINYI MLIPOFIKA. Ninyi ndio WATU PEKEE nitakaowaambia.

Wao walitamani kuyajua na kuyasikia mambo haya yote ya ajabu ambayo nimeyaficha, lakini kama vile nilivyokuahidi, nimesubiri na kuyaweka kuwa siri hadi hivi sasa, kwa ajili yako WEWE tu, WANGU MMOJA NA WA PEKEE.

Nilikuahidi Mimi ningekuja na kujifunua Mwenyewe tena katika mwili wa mwanadamu, ili niweze kukuambia, na kukufunulia mambo haya yote. Nilitaka uisikie SAUTI YANGU ikizungumza nawe moja kwa moja.

Nimewatia mafuta wengine wengi kwa Roho Wangu Mtakatifu kukuambia kuhusu upendo Wangu, lakini kama nilivyofanya siku zote, Nami kamwe siwezi kubadilika, nilimchagua mtu mmoja: Malaika Wangu, Nabii Wangu, awe Sauti Yangu ili niweze kunena Bwana Asema Hivi kwako.

Nilitaka kukuambia, wewe hukuokolewa siku yoyote Maalum. Daima ulikuwa umeokolewa. Nilikuja tu kukukomboa. Uliokolewa tangu mwanzo kwa maana ulikuwa na Uzima wa Milele, kwanza. Kwa hivyo, machoni Pangu, dhambi zako zote haziwezi hata kuonekana Nami, kitu pekee ninachosikia ni sauti yako. Ninauona tu uwakilisho wako.

Jinsi gani nimesubiri kwa hamu kukuambia mambo mengi. Moyo wangu unabubujika kwa shauku. Jinsi gani nimeisubiri kwa hamu Karamu yetu ya Harusi, Miaka elfu moja ya Utawala wetu Wa Miaka Elfu tukiwa pamoja. Nikikuambia kwa undani kuhusu Makao Yetu ya Baadaye pamoja; Jinsi nilivyokuandalia kila kitu, kila kitu jinsi tu unavyopenda hasa.

Kipenzi Changu, ikiwa unaona ni vizuri mno sasa hivi kuisikiliza Sauti yangu ikizungumza nawe, subiri tu, hiki ni kivuli tu cha jinsi itakavyokuwa wakati tutakapoishi Katika ule Mji pamoja. Nabii wako yeye hata ataishi karibu nawe; atakuwa jirani yako.

Tutatembea kwenye barabara hizo za dhahabu na kunywa kutoka kwenye chemchemi pamoja. Tutatembea katika paradiso za Mungu huku Malaika wakiizunguka dunia, wakiimba nyimbo za sifa….Itakuwa ni Siku ya namna gani!

Najua njia inaonekana inaparuza, na wakati mwingine inakuwa ngumu kwako, lakini itakuwa kitu kidogo sana, kidogo sana, Tutakapokuwa pamoja.

Kwa sasa, nitakukusanya Kwa mara nyingine tena na kuzungumza nawe Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville, (ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) na kukuambia kila kitu kuhusu “Makao Ya Baadaye Ya Bwana Arusi wa Mbinguni na Bibi-arusi wa Duniani”. Nasubiri kwa hamu kuungana nawe wakati huo.

Kumbuka, na kamwe usisahau, nakupenda sana.

Kwa niaba Yake,

Ndugu Joseph Branham

Maandiko:
Mathayo Mt. 19:28
Yohana Mt. 14: 1-3
Waefeso 1:10
2 Petro 2:5-6 / Sura ya 3
Ufunuo 2:7 / 6:14 / 21:1-14
Walawi 23:36
Isaya Sura ya 4 / 28:10 / 65:17-25
Malaki 3:6

26-0104 Mabirika Yavujayo

UJUMBE: 64-0726E Mabirika Yavujayo

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wanywaji Wa Kisima Kinachofoka Maji,

Ni Krismasi na Mwaka Mpya ulioje tuliokuwa nao. Tumezikubali na kuzifungua zawadi za Mungu alizomtumia Bibi-arusi Wake. Zawadi yetu ya kwanza ilikuwa ni Zawadi kuu kuliko zote ya Krismasi iliyowahi kufungwa. Mungu Mwenyewe alijifunga Mwenyewe katika mwili wa mwanadamu na akakituma kifurushi hicho duniani. Ilikuwa ndio Zawadi Yake kubwa sana ya kwanza ya kumrejesha Bibi-arusi Wake.

Kisha Mungu akakituma kifurushi kingine kikubwa kwa Bibi-arusi Wake. Yeye alitupenda sana hivi kwamba alikuja na kujifunua Mwenyewe katika mwili tena ili aweze kuzungumza nasi mdomo kwa sikio. Alitaka Yeye na Bibi-arusi Wake wawe Mmoja.

Na sasa, enyi marafiki, msinielewe vibaya. Naomba niliseme hili kwa heshima moyoni mwangu, nikijua kwamba mimi ni mtu ninayeelekea kwenye Umilele ambaye nitasimama mbele ya Hukumu siku moja: Maelfu ya watu wanaikosa zawadi yao waliotumiwa. Unaona? Hawawezi kuielewa. Nao wanaangalia, na kusema, “Loo, yeye ni mtu tu.” hiyo ni kweli. Je, ilikuwa ni Mungu au Musa aliyewaokoa wale watu? Ilikuwa ni Mungu ndani ya Musa. Unaona? Wao walimlilia mkombozi. Na wakati Mungu alipowatumia huyo mkombozi, walishindwa kuliona, kwa sababu ilikuwa kupitia mtu, lakini haikuwa huyo mtu, ilikuwa ni Mungu ndani ya mtu huyo.

Leo, kwa mara nyingine tena, maelfu ya watu wanaikosa zawadi yao na kusema, “huna haja ya kusikiliza kanda, hivi sasa kuna watu wengine waliotiwa mafuta,” ambayo ni kweli, lakini wao wanashindwa kutambua kuwa hiyo ndio Sauti PEKEE iliyothibitishwa na Mungu, inenayo Bwana Asema Hivi kupitia mtu huyo. Sauti hiyo ndio Urimu na Thumimu ya Mungu, Yakini Yake ya wakati huu.

Tunapoisikiliza Sauti Yake iliyo kwenye kanda tunakunywa kweli kutoka kwenye Kisima cha Mungu kinachofoka maji, ambacho hakihitaji kuvuta kwa mashine, kuvuta, kujiunga, kuteka; sisi tunaamini tu na kutegemea kila Neno Linalonenwa.

Kwa sisi kuisikiliza Sauti hiyo iliyo kwenye kanda, kulingana na Yesu Mwenyewe, tunao ushahidi wa kweli wa Roho Mtakatifu katika siku yetu.

Kwa hiyo huo hapo ushahidi halisi wa Roho Mtakatifu! Yeye hajaniambia bado jambo lo lote ambalo si sahihi. Ya kwamba, “Ni ushahidi wa Roho Mtakatifu, ni yeye yule anayeweza kuliamini Neno.” kama unaweza kulipokea.

Mungu ametuandalia Chemchemi tunayoweza kuinywea kila dakika ya kila siku. Daima ni safi. Si kitu fulani kilichooza, Ni Chemchemi Yake isiyokauka, inayojitegemea; unatakiwa tu Ubonyeze Play.

Tukinena kuhusu ZAWADI kutoka kwa Mungu, Je, unaweza kuwazia kweli jinsi gani Zawadi hii ilivyo KUU? Kwa Kubonyeza play tu na kuisikiliza Sauti Yake iliyo kwenye kanda, ndiyo pekee… SAUTI PEKEE duniani ambayo huhitaji chujio, kichujio, au chochote kile. Unatakiwa tu kusikiliza, kuamini, na kusema amina kwa kila Neno.

Mungu Mwenyewe ameiandaa njia hii, NJIA YAKE PEKEE, ya kupokea uzima wa milele, na muhimu zaidi, YA KUWA BIBI-ARUSI WAKE. Tunaweza tu kulala kifuani Mwake na kuzinyonya nguvu zetu kwa kuisikiliza Chemchemi Yake, Sauti Yake, El Shaddai akizungumza na Bibi-arusi Wake.

Hebu mwaka huu na uwe ndio mwaka atakaokuja kutuchukua, sisi Bibi-arusi Wake mpendwa. Tunatazamia na kungoja kwa matarajio makubwa. Siku yoyote hivi sasa tutawaona wale ambao tumetamani kuwaona wakitokea. Tutatambua, Katika kufumba na kufumbua jicho, tutakuwa tumetoka mahali hapa, tumeitwa kwenda kwenye Karamu yetu ya Harusi.

Bwana, tuonapo meza hiyo kubwa imetandazwa pale kwa ajili ya hiyo karamu, maelfu ya maili, tukitazamana, askari wa vita walio na majeraha, machozi ya furaha yakitiririka mashavuni mwetu… Mfalme akijitokeza katika uzuri Wake, utakatifu, ashuke mezani na kuchukua mikono Yake Mwenyewe na kuyafuta machozi kutoka machoni mwetu, akisema, “Msilie tena, yote yamekwisha. Ingieni katika raha za Bwana.” Taabu za safarini hazitaonekana kuwa kitu wakati huo, Baba, tutakapofika kwenye mwisho wa njia.

Njoo unywe, unywe, unywe, unywe pamoja nasi kutoka kwenye Chemchemi iliyoandaliwa na Mungu ya siku hii Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville. (ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) Ndio mahali PEKEE ambapo unaweza kupumzika kabisa na kusema AMINA kwa kila Neno usikialo. Ndicho kisima Chake kinachofoka maji kilichoandaliwa ili Bibi-arusi Wake apate kukinywea.

Ndugu. Joseph Branham

Ujumbe: 64-0726E Mabirika Yavujayo

Maandiko ya kusoma kabla ya kuusikiliza Ujumbe:
Zaburi 36:9
Yeremia 2:12-13
Yohana 3:16
Ufunuo Sura ya 13

25-1228 Kutambua Siku Yako Na Ujumbe Wake

UJUMBE: 64-0726M Kutambua Siku Yako Na Ujumbe Wake

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi Aliyekatwa Akatolewa,

Leo, kanisa limemsahau nabii wao. Hawamhitaji yeye tena ahubiri katika makanisa yao. Wanadai wana wachungaji wao wa kuwahubiria na kuwanukulia na kuwafasiria Neno. Kuhubiri ni muhimu zaidi kuliko kuisikiliza Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda katika makanisa yao.

Bali Mungu alijua Yeye hana budi kuwa na nabii Wake; hivyo ndivyo Yeye amekuwa akimwita atoke na kumwongoza Bibi-arusi Wake kila wakati. Yeye Alitukata akatutoa kutoka miongoni mwa mataifa mengine kwa Upanga Wake wenye makali kuwili, Roho Wake Mtakatifu, Sauti Yake iliyonenwa na nabii Wake.

Yeye ametukata kwa Sauti hiyo. Ndiyo maana aliirekodi na kuiweka kwenye kanda. Kwa Ufunuo tunaona jinsi Maandiko yalivyo makamilifu! Bibi-arusi hawezi kuivishwa isipokuwa Mwana aiivishe.

Haidhuru utahubiri namna gani, hata ufanye nini, haliwezi kuivishwa, haliwezi kudhihirishwa, haliwezi kuthibitishwa; ila tu na Yeye aliyesema, “Mimi Ndimi Nuru ya ulimwengu,” lile Neno.

Neno lilituambia Roho Mtakatifu Mwenyewe atatokea na kutuivisha, ili kuthibitisha, kuhakikisha na kujidhihirisha. Nuru ya jioni imekuja. Mungu akijidhihirisha Mwenyewe katika mwili ili kumwita Bibi-arusi Wake atoke.

Yeye Ndiye aliyekuita WEWE utoke kwa Roho Wake Mtakatifu, Neno Lake, Sauti Yake. Yeye Ndiye aliyekuchagua WEWE. Yeye Ndiye anayekufundisha WEWE. Yeye Ndiye anayekuongoza WEWE. Kwa kitu gani? Roho Wake Mtakatifu, Sauti Yake ikizungumza NA WEWE MOJA KWA MOJA.

Lakini kwao Hilo limepitwa na wakati sana katika siku hii. Wamepita muda wa kuzicheza kanda makanisani mwao. Wao hawalitambui. Hiyo ndiyo sababu wako katika hali waliyo nayo. Lakini kwako wewe, imefunuliwa Kuwa ndio njia ya Mungu Iliyoandaliwa, NI BWANA ASEMA HIVI KWAKO.

Kwa hiyo hakuna budi kutokee Nguvu fu—fu—fulani, Roho Mtakatifu Mwenyewe, kuivisha, ama kuthibitisha, ama kuhakikisha, ama kudhihirisha ya kwamba yale ambayo Yeye amebashiri yangetukia katika siku hii. Nuru ya jioni inaleta hilo. Ni wakati wa jinsi gani!

Sisi ndiye Bibi-arusi Neno mkamilifu ambaye nabii Wake alimwona katika ono. Sisi ndio wale ambao Yeye alimtuma nabii Wake kuwaita watoke kwa Neno Lake, na sasa tunao UAMSHO, kwa maana sasa tunajua sisi ni nani.

Kufufua, hapo, ni neno lile lile linalotumika mahali pengine popote, ndiyo kwanza nilichunguze, linamaanisha, “uamsho.” “Yeye atatufufua baada ya siku mbili.” Hiyo ingekuwa, “Katika siku ya tatu Yeye atatufufua tena, baada ya kututawanya, na kutupofusha, na kuturarua.”

Baba alimtuma nabii Wake kumwangalia Bibi-arusi Wake ili kwamba tusitoke mstarini. Kumbuka, hili lilikuwa ono!

Bibi-arusi alipitia mahali pale pale alipopitia wakati alipokuwa hapo mwanzo. Lakini nilikuwa nikimwangalia akitoka mstarini, na nikijaribu kumvuta arudi kwenye mstari.

Lakini “yeye” angewezaje kumvuta arudi mstarini leo? “Yeye”, mtu huyo, hayupo hapa duniani. KWA NENO! Neno PEKEE lililothibitishwa la wakati huu ni lipi? Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda.

Wahudumu wameitiwa kulihubiri Neno kwa kunukuu kile hasa nabii alichosema. Kulingana na nabii mwenyewe, wao hawapaswi kusema chochote zaidi.

Kweli, wameitiwa kulifundisha na kulihubiri Neno hilo. Lakini kuna SAUTI MOJA PEKE YAKE ILIYOTHIBITISHWA NA MUNGU MWENYEWE KUWA BWANA ASEMA HIVI.

Nasema vivyo hivyo katika Jina la Yesu Kristo. Usiongeze kitu. Usiondoe—kuliwekea mawazo yako. Wewe sema tu yaliyosemwa katika kanda hizo. Tenda sawasawa kabisa na vile Bwana Mungu amekuamuru kutenda. Usiongezee Kwake!

Kama ukisema “amina” kwa kila neno ambalo mchungaji wako au mhudumu wako asemalo, umepotea. Lakini ukisema “AMINA” KWA KILA NENO AMBALO MUNGU ALILOLINENA KUPITIA NABII WAKE KWENYE KANDA, WEWE NDIYE BIBI-ARUSI NA UTAKUWA NA UZIMA WA MILELE.

Nabii wa Mungu alikuwa ndiye mtu ambaye Mungu alimchagua kuzungumza kupitia yeye. Ilikuwa ni CHAGUO LA MUNGU kumtumia yeye kulinena Neno Lake na kuliweka kwenye kanda ili kwamba Bibi-arusi angekuwa SIKU ZOTE NA BWANA ASEMA HIVI YA KUSIKIA.

Yeye hataki Bibi-arusi Wake ategemee kile watu wengine wasemacho, au fasiri yao ya Neno Lake. Yeye anataka Bibi-arusi Wake asikie kutoka kwenye midomo Yake hadi masikioni mwao. Yeye hataki Bibi-arusi Wake amtegemee mtu mwingine yeyote ila Yeye Mwenyewe.

Tunapoamka asubuhi, tunapenda Yeye atuambie, “Habari za asubuhi marafiki. Nitazungumza nanyi leo na kuwaambieni jinsi gani ninavyowapenda na jinsi ambavyo ninyi na Mimi tulivyo MMOJA. Ninao wengi ambao nitakaowapa uzima wa milele, bali ni WEWE peke yake ndiye Bibi-arusi niliyemchagua kwa mkono Wangu. WEWE peke yake ndiye niliyempa Ufunuo kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu.

Wengine wengi wanapenda kunisikia, lakini Mimi nimewachagua ninyi kuwa Bibi-arusi Wangu. Kwa maana mmenitambua Mimi nanyi mmedumu na Neno Langu. Hamjapatana, hamjabembana, bali mmedumu waaminifu na Neno Langu.

Muda umekaribia. Ninakuja kuwachukua hivi karibuni. Kwanza, mtawaona wale walio pamoja nami sasa. Loo, jinsi wao wanavyotamani kuwaona na kuwa pamoja nanyi. Msihofu enyi watoto, kila kitu kiko kikamilifu kwenye wakati unaofaa, endeleeni tu kusonga mbele.”

Kama mhudumu wa Injili, siwezi kuona jambo moja lililosalia ila kule kuondoka kwa Bibi-arusi.

Ndugu. Joseph Branham

Ujumbe: 64-0726M “Kutambua Siku Yako na Ujumbe Wake”

Muda: saa 6:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki)

Maandiko ya kusoma kabla ya kuusikia Ujumbe:
Hosea: Sura ya 6
Ezekieli: Sura ya 37
Malaki: 3:1 / 4:5-6
Timotheo wa Pili: 3:1-9
Ufunuo: Sura ya 11

25-1221 Kuenda Nje Ya Kambi

UJUMBE: 64-0719E Kuenda Nje Ya Kambi

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Laazizi Mpendwa,

Mungu habadiliki. Neno Lake halibadiliki. Mpango Wake haubadiliki. Na Bibi-arusi Wake habadiliki, tutadumu na Neno. Ni zaidi ya uhai kwetu; Ni chemchemi ya Maji Yaliyo Hai.

Kitu pekee tulichoagizwa kufanya ni kulisikia Neno, ambalo ni Sauti ya Mungu iliyothibitishwa ambayo imerekodiwa na kuwekwa kwenye kanda. Kitu pekee tunachokiona si kanuni ya imani, si kundi la watu, hatuoni kitu kingine ila Yesu, Naye ni Neno lililofanyika mwili katika siku yetu.

Mungu yuko katika Kambi yetu nasi tuko njiani kuelekea Utukufuni tukiongozwa na Nguzo ya Moto, ambayo ni Mungu Mwenyewe akizungumza kupitia nabii Wake aliyethibitishwa wa Malaki 4. Tunakula ile Mana iliyofichwa, Maji Yaliyo Hai ambayo ni Bibi-arusi peke yake ndiye anayeweza kula.

Mungu habadilishi njia Zake, na wala shetani habadilishi zake. Kile alichofanya miaka 2000 iliyopita, yeye anafanya jambo lile lile leo, isipokuwa tu amekuwa mwerevu zaidi.

Sasa, baada ya miaka mia nne, Mungu alitembea moja kwa moja miongoni mwao siku moja. Kulingana na Maandiko, Yeye alikuwa afanyike mwili na akae miongoni mwao. “Jina Lake ataitwa Mshauri, Mfalme wa Amani, Mungu mwenye Nguvu, Baba wa Milele.” Na wakati alipokuja miongoni mwa watu, wao walisema, “Hatutaki Mtu huyu atutawale!….”

Kulingana na Maandiko, Mwana wa Adamu angekuja kwa mara nyingine tena na kuishi na kujifunua Mwenyewe katika mwili wa mwanadamu, Naye alifanya hivyo, nao wanasema kitu kile kile. Hakika, wanaunukuu na kuuhubiri Ujumbe, lakini hawatataka mtu huyo awatawale.

Hiki ndicho hasa kinachotendeka:

Na kama ilivyokuwa wakati huo, ndivyo ilivyo leo! Biblia ilisema kanisa la Laodikia lingemtupa nje, Naye alikuwa anabisha, akijaribu kuingia. Kuna kasoro mahali fulani. Sasa, kwa nini? Walikuwa wamefanya kambi yao wenyewe.

Mtu anaweza kusema, “Ninajua na ninaamini Ndugu Branham alikuwa nabii. Alikuwa ndiye malaika wa saba. Alikuwa ndiye Eliya. Tunauamini Ujumbe huu. Kisha kutoa aina fulani ya udhuru, wowote ule uwao, wa kutoicheza Sauti PEKEE ya Mungu iliyothibitishwa kanisani mwao… Kuna kasoro mahali fulani. Sasa, kwa nini? Walikuwa wamefanya kambi yao wenyewe.

Ninayasema mambo haya si kulitenganisha kanisa, Neno la Mungu ndilo linalofanya jambo hilo. Mimi Nataka tuungane pamoja, tuwe KITU KIMOJA sisi kwa sisi na pamoja Naye, lakini kuna njia moja tu ya kufanya hivyo: kwenye Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda. Hiyo ndio BWANA ASEMA HIVI PEKEE.

Mungu ametufunulia njia Yake kamilifu kwetu. Ni tukufu sana na hata hivyo ni rahisi sana. Kila Ujumbe tunaousikia akituambia, anatuhakikishia, anatutia moyo, kwamba SISI NDIO BIBI-ARUSI WAKE. Tuko katika mapenzi Yake makamilifu. Tumejiweka wenyewe tayari kwa KUMSIKIA YEYE.

Ujumbe huu ni wa hivi sasa kuliko gazeti la kesho. Sisi ni unabii unaotimizwa. Sisi ni Neno lililodhihirishwa. Mungu anatuthibitishia kwa kila Ujumbe tunaousikia kwamba leo, Maandiko haya yanatimizwa.

Yawezekana kuwe na baadhi huko nje katika mataifa, ulimwenguni kote, ambao hata kanda hii ingewakuta manyumbani mwao au makanisani mwao. Tungeomba, Bwana, kwamba wakati ibada inaendelea, pale—pale… au kanda inachezwa, au nafasi yo yote tunayoweza kuwamo, au—au hali, yule Mungu mkuu wa Mbinguni na aheshimu huu unyofu wa mioyo yetu asubuhi hii, na kuponya wahitaji, kuwapa wao yale wanayohitaji.

Hebu Subiri kidogo…. hivi Sauti ya Mungu kwa ulimwengu imetoka kutabiri nini na kusema nini?…. watu wangekuwa wakicheza kanda majumbani mwao au makanisani mwao.

Lakini tunakosolewa na kukemewa Kwa kusema ati HATUWEZI kuwa na Kanisa la Kanda la Nyumbani? Ati Ndugu Branham hakuwahi kusema chezeni kanda MAKANISANI mwenu?

UTUKUFU KWA MUNGU, LISIKIE, LISOME, NI BWANA ASEMA HIVI. Na si tu kwamba YEYE alilisema hilo, bali kwa kuzicheza kanda majumbani mwenu na makanisani MWENU, Yule Mungu mkuu wa Mbinguni ataheshimu unyofu wa mioyo yetu na kuwaponya wahitaji na kutupa YOYOTE YALE TUNAYOHITAJI!!

Hii nukuu moja INATHIBITISHA kwamba hawa watu wanawasikiliza wachungaji wao na HAWALISIKII NENO, la sivyo wangewapa changamoto na kuwathibitishia kwa NENO kwamba sisi tuko katika MAPENZI YAKE MAKAMILIFU, na kuko katika MAPENZI YAKE MAKAMILIFU KUZICHEZA KANDA KATIKA MAKANISA YAO.

Siliweki mahali pasipo pake au kulinukuu vibaya Neno kama wengi wasemavyo ati nafanya. Lisikie na ulisome wewe mwenyewe.

Ni rahisi sana na kamilifu sana, BONYEZA PLAY na uisikie Sauti ya Mungu ikizungumza nawe. Sema “Amina” kwa kila Neno usikialo. Hata huna haja ya kulielewa, wewe yakupasa tu kuliamini.

“Nataka kwenda nje ya kambi. Haidhuru itanigharimu nini, nitautwaa msalaba wangu na kuubeba kila siku. Nitatoka nje ya kambi. Hata watu waseme nini juu yangu, nataka kumfuata nje ya kambi. Niko tayari kwenda.”

Njoo upite kizuizi cha sauti uingie kwenye Neno la Mungu pamoja nasi Jumapili hii saa 6:00 MCHANA, saa za Jeffersonville.(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) Hayapimiki yale Mungu anayoweza na atakayofanya na mtu ambaye yuko tayari kwenda nje ya kambi ya mwanadamu.

Ndugu Joseph Branham

Ujumbe: 64-0719E Kuenda Nje Ya Kambi

Maandiko: Waebrania 13:10-14 / Mathayo 17:4-8

25-1214 Sikukuu Ya Baragumu

UJUMBE: 64-0719M Sikukuu Ya Baragumu

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi Mkamilifu,

Hili si jambo tu la kujibunia, enyi marafiki. Hii ni BWANA ASEMA HIVI, Maandiko.

Kila Mkristo anataka kuwa Bibi-arusi, lakini tunajua Bibi-arusi Wake watakuwa wachache tu waliochaguliwa. Tunajua Yeye anayo mapenzi ya kuruhusia, lakini Bibi-arusi Wake lazima awe katika mapenzi Yake makamilifu. Kwa hivyo, lazima tumtafute Mungu katika Neno Lake, na kisha kwa Ufunuo, tutajua mapenzi Yake makamilifu jinsi ya kuwa Bibi-arusi Wake.

Tunapaswa kuyachunguza Maandiko, kwa maana tunajua Mungu KAMWE Habadilishi mawazo Yake kuhusu Neno Lake. Mungu habadilishi mpango Wake. Yeye habadilishi CHOCHOTE. Jinsi alivyofanya mara ya kwanza ni kamilifu. Kile Yeye alichofanya jana atafanya vivyo hivyo leo.

Jinsi Yeye alivyomwokoa mwanadamu tangu mwanzo, itambidi amwokoe mtu leo kwa njia ile ile. Jinsi Yeye alivyomponya mtu wa kwanza, hana budi kufanya vivyo hivyo leo. Jinsi ambavyo Mungu alichagua kumwita na kumwongoza Bibi-arusi Wake, atafanya vivyo hivyo leo; kwa kuwa Yeye ni Mungu na hawezi kubadilika. Neno linatuambia kwamba Yesu Kristo ni YEYE YULE jana, leo na hata milele.

Kwa hivyo, wakati tunapolisoma Neno Lake, tunaweza kuona wazi kabisa Jinsi Yeye alivyochagua kumwita na kumwongoza Bibi-arusi Wake kwa kila kizazi. Yeye Alimchagua MTU MMOJA. Alisema wao walikuwa Neno la siku yao. Nabii alituambia Yeye KAMWE hakuwa na kundi la watu; wao wana njia tofauti, mawazo tofauti, na muhimu zaidi, alisema, NENO LA MUNGU HALIHITAJI KUFASIRIWA.

Kwa hivyo, kile kila nabii alichosema katika kila kizazi hakiwezi kuongezwa kwake au kuondolewa. Lazima iwe Neno kwa Neno kile ALICHONENA. Rahisi sana ukiniuliza mimi Njia ya Mungu iliyoandaliwa ni ipi….DUMU NA NABII.

Sasa, sio tu kwamba tunajua fika njia ya Mungu iliyoandaliwa tangu mwanzo vile imekuwa, bali Bwana Yeye hata atanena kupitia malaika Wake na kutuambia kile Yeye atakachofanya katika siku zijazo, ili tu kuthibitisha kwa mara nyingine tena, MUNGU HABADILISHI MPANGO WAKE.

Baada ya Bibi-arusi Wake (sisi) kuondoka hapa duniani na kuitwa kwenda kwenye Karamu ya Harusi, Mungu atawaitaje wale Wayahudi 144,000 waliochaguliwa? Kundi la watu?

Sasa, mara Kanisa hili (Bibi-arusi) limevutwa pamoja, linanyakuliwa; na ile siri ya Muhuri ya Saba, ama Muhuri ya Saba, ile siri ya kuondoka. Nao Wayahudi wanaitwa kwa siri ya Baragumu ya Saba, ambayo ni manabii wawili, Elia na Musa, nao wanarudi.

Kwa hivyo mara tu Bibi-arusi atakapovutwa pamoja, tutatwaliwa juu. Tunajua kuna kitu kimoja tu kinachoweza kumvuta Bibi-arusi pamoja, Roho Mtakatifu, Naye Roho Mtakatifu ni Neno Lake, nalo Neno Lake la siku hii ni Sauti ya Mungu, nayo Sauti ya Mungu ni…

Kama nimewaudhi kwa kusema hivyo, nisameheni, lakini, nilihisi hilo huenda lilichukiwa, bali, mimi ni Sauti ya Mungu kwenu. Mnaona? Nalisema hilo tena, wakati huo ilikuwa chini ya uvuvio, mnaona.

Naomba niingilie hapa na niseme, NUKUU hii MOJA tu kutoka kwa malaika-mjumbe wa Mungu aliyethibitishwa inapaswa kutosha kabisa kwa wote wanaojiita waaminio katika Ujumbe huu wa wakati wa mwisho wadai mchungaji wao ABONYEZE PLAY katika makanisa yao au ajiuzulu ili waweze kumpigia kura mchungaji mwenye UFUNUO WA KWELI KUTOKA KWA MUNGU.

Kwa hivyo, Baragumu ilipigwa nao manabii wawili wakatokea kwani Yeye hawezi kuwa na malaika Wake wa saba pamoja na Bibi-arusi Wake hapa duniani wakati ule ule wao wanapokuja. Kwa hivyo Yeye anawaitaje Wayahudi? Kwa njia ile ile aliyomwita Bibi-arusi Wake Mmataifa.

Nao Wayahudi wanaitwa kwa siri ya Baragumu ya Saba, ambayo ni manabii wawili…

Bibi-arusi hana budi kuondoka njiani, apate kwenda juu sasa; kusudi wale watumishi wawili, wale watumishi wawili wa Mungu, katika Ufunuo, wale manabii wawili, wapate kujitokeza, kusudi wawapigie ile Baragumu ya Saba, wawajulishe Kristo.

Ni wazi kabisa, Mungu habadilishi mpango Wake. Yeye aliwatuma manabii Wake. Kwa hivyo, Bibi-arusi Wake atadumu na njia Yake iliyoandaliwa, nabii-malaika Wake, Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda.

Kisha ili kulifanya liwe wazi kabisa, Mungu kwa mara nyingine tena anazungumza na kumwambia Bibi-arusi Wake: Mmedumu waaminifu Kwangu na njia Yangu iliyoandaliwa, kwa hivyo njia Yangu iliyoandaliwa ya siku yenu itawaambieni:

Yule malaika wa saba, mjumbe, aseme, “Tazama Mwana-Kondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu!”

SAUTI HIYO ni muhimu sana; SAUTI YA MUNGU ikinena kupitia malaika Wake wa saba kwenye kanda. Mungu ataitumia SAUTI HIYO, SAUTI YA MALAIKA WAKE WA SABA. SIO KUNDI…SIO MIMI…SIO MCHUNGAJI WAKO…SAUTI YA MALAIKA-MJUMBE WAKE WA SABA kututambulisha sisi Kwake, Bwana wetu Yesu Kristo.

Kwa hivyo, tunafahamu:

  • SISI NDIO BIBI-ARUSI WAKE.
  • TUKO KATIKA MAPENZI YAKE MAKAMILIFU.
  • TUNAUFUATA MPANGO WAKE KWA AJILI YA SIKU HII KWA KUBONYEZA PLAY.

Sehemu ya Bibi-arusi Wake itakusanyika Jumapili hii saa 6:00 MCHANA, masaa ya Jeffersonville,(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki) kumsikiliza mchungaji wetu, malaika- mjumbe wa Mungu, William Marrion Branham, Naye atakuwa akizungumza nasi na kutufunulia kwamba halipo kanisa lingine, hamna kundi lingine la watu tangu kuumbwa kwa ulimwengu, ambalo limewahi kupata fursa tuliyonayo ya kuungana pamoja kumsikiliza Mungu akizungumza nao moja kwa moja.

Sisi ni watu waliobarikiwa Jinsi gani. Tunayo furaha sana. Tunashukuru sana. Bibi-arusi anafanyika MMOJA na Bwana-Arusi

Ndugu Joseph Branham

Sikukuu Ya Baragumu 64-0719M.

Maandiko ya kusoma kabla ya Kusikiliza Ujumbe:
Mambo ya Malawi 16
Mambo ya Walawi 23:23-27
Isaya 18:1-3
Isaya 27:12-13
Ufunuo 10:1-7
Ufunuo 9:13-14
Ufunuo 17:8

25-1207 Ndipo Yesu Akaja Na Kuita

UJUMBE: 64-0213 Ndipo Yesu Akaja Na Kuita

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi Neno,

Tunaishi katika saa zenye giza kuliko, lakini sisi HATUNA HOFU, Bwana amekuja. Amekuja kulitimiza Neno Lake katika siku ya mwisho. Jinsi Alivyokuwa wakati huo, ndivyo Alivyo leo. Jinsi udhihirisho na utambulisho Wake ulivyokuwa wakati huo, ndivyo ulivyo leo. Yeye angali ni Neno la Mungu, akijidhihirisha Mwenyewe katika mwili wa kibinadamu katika malaika Wake wa saba mwenye nguvu na ametufunulia, sisi ni Bibi-arusi Neno lililo Hai Wake.

Hatuna muda wa kujadiliana au kuzozana; tumepita wakati huo; tunasonga mbele, inatupasa kufika kule. Roho Mtakatifu amekuja miongoni mwetu. Bwana Yesu katika umbo la Roho amejifunua na kujidhihirisha Mwenyewe kupitia nabii Wake kwamba Yeye ni Sauti ya Mungu kwa Bibi-arusi Wake.

Yeye alisema angekuja. Alisema angefanya jambo hili. Alisema angejitokeza jukwaani katika siku za mwisho na kufanya mambo haya kama alivyofanya alipokuja katika mwili mara ya kwanza, Naye huyu hapa akilifanya jambo hilo. Mnaogopa nini? HAKUNA!!!

Tumo njiani kuelekea Utukufuni! Hakuna kitu kitakachotukomesha. Mungu atalithibitisha Neno Lake. Sijali ni kitu gani kitakachotukia. Wakati wa matendo umefika. Wakati wa kuamini ama kutokuamini umefika. Ule Mstari wa kutengana ambao huwajia kila mwanamume na mwanamke umewasili.

Wewe ulizaliwa kwa kusudi fulani. Wakati Nuru ilipokumulika, iliondoa giza lote ndani yako. Wakati ulipoisikia Sauti Yake ikizungumza nawe kwenye kanda, jambo fulani lilitendeka. Ilinena na nafsi yako. Ilisema, “Bwana amekuja na anakuita. Usifadhaike, usiogope, Ninakuita. Wewe ni Bibi-arusi Wangu”.

Enyi watu, iweni na hakika! Msibahatishe tu nusunusu kuhusu hilo. Mungu anao mpango: Neno Lake alilolirekodi kwenye kanda. Bwana amekuja na anawaita. Njooni kwenye njia ya Mungu iliyoandaliwa.

Bwana atamuunganisha kwa mara nyingine tena Bibi-arusi Wake kote ulimwenguni na Sauti Yake. Atatutia moyo, atatuhakikishia, atatuponya, atatuleta katika Uwepo Wake mkuu na kutuambia:

Bwana amekuja na anakuita. Loo, ewe mwenye dhambi, loo, ewe mgonjwa, hivi huoni Bwana aliyedhihirishwa katika mwanadamu, katikati ya waamini? Yeye amekuja kuwaita watoto Wake wanaoamini wapate afya. Amekuja kumwita mwenye dhambi apate kutubu. Ewe uliyerudi nyuma, mfuasi wa kanisa, Bwana amekuja na anakuita.

Ni kumwagwa kwa Roho Wake Mtakatifu kulikoje ambako Bibi-arusi atakuwanako Jumapili hii Mungu atakapowakusanya watoto Wake pamoja Kwa mara nyingine tena na kuingia katika nyumba zetu, makanisa yetu, mikusanyiko yetu, na kutuita na kusema, “Bwana amekuja na anawaita. Chochote mnachokihitaji, ni chenu.”

Hebu maneno hayo na yaingie ndani ya mioyo yenu, ndugu na dada. CHOCHOTE MNACHOKIHITAJI, BWANA AMEKUJA NA KUWAPENI JAMBO HILO.

Baba wa Mbinguni, Ee Bwana, jalia litukie tena. Mambo yote hayo ambayo nimesema, “Yesu amekuja na anakuita.” Yeye hufanya nini hapo anapokuja? Huita. Na jalia litendeke tena, Bwana. Jalia Roho Wako Mtakatifu aje miongoni mwa watu usiku wa leo, Bwana Yesu katika umbo la—la Roho. Jalia aje usiku wa leo na ajifunue Mwenyewe, halafu ajidhihirishe Mwenyewe.

Ndugu Joseph Branham

Ujumbe: 64-0213 Ndipo Yesu Akaja Na Kuita
Saa: 6:00 MCHANA masaa ya Jeffersonville(ni saa 2:00 USIKU ya Afrika Mashariki)

Maandiko:Yohana Mt. 11:18-28

25-1130 Kile Kipeo

UJUMBE: 64-0705 Kile Kipeo

PDF

pakua – m4a

pakua – amr

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Kipeo Cha Mungu,

Uhai wote wa kweli uliokuwemo Katika ubua, kishada, na ganda, sasa unakusanyika ndani yetu, Uzao wa Kifalme wa Mungu, Vipeo Vyake, nasi tuko kwa ufufuo, tayari kwa mavuno. Alfa imekuwa Omega. Ya kwanza imekuwa ya mwisho, na ya mwisho sasa ndiyo ya kwanza. Tumepitia hatua fulani nasi tumekuwa Vipeo Vyake, kipande kilichokatwa kutoka Kwake.

Bibi-Arusi na Bwana-Arusi ni Mmoja!

Mungu alimwonyesha nabii Wake kule kuonekana kimbele kwa kila mmoja wetu tupate kukaguliwa, Vipeo Vyake, katika ono. Aliposimama pale na Bwana akimtazama Bibi-Arusi akipita mbele yake, Yeye Alimwona kila mmoja wetu. Sisi SOTE macho yetu yalikuwa yameelekezwa MOJA KWA MOJA KWAKE YEYE. Alisema tulikuwa watu walio wazuri mno aliopata kuwaona maishani mwake. Tulikuwa na madaha. Tulionekana wazuri mno kwake.

Kumbukeni, hili lilikuwa ni ONO la Bibi-Arusi; vile angeonekana, na kutuambia hasa kile alichokuwa akifanya. Sikilizeni kwa makini.

Yeye atatoka katika mataifa yote, kumkamilisha Bibi-arusi. Kila mmoja wao alikuwa na nywele ndefu na bila kujipodoa, nao ni wasichana wazuri sana. Nao walikuwa wakinitazama. Hao waliwakilisha Bibi-arusi akitoka katika mataifa yote. Mnaona? Yeye…Kila mmoja wao aliwakilisha taifa moja,* walipokuwa wakipiga hatua kikamilifu kulingana na Neno.

Bibi-Arusi, Hebu niliseme hilo tena, BIBI-ARUSI, kutoka kila taifa ati walikuwa wameyaelekeza macho yao kwa mchungaji wao, kundi la watu….HAPANA, hivyo sivyo alivyosema. Wao walikuwa wameyaelekeza macho yao KWA NABII, wakimtazama yeye.
Mradi tu waliyaelekeza macho yao kwa nabii, walikuwa wakipiga hatua kikamilifu. Lakini Kisha yeye anatuonya, jambo fulani lilitukia. Baadhi yao waliyaondoa macho yao kwake na kuanza kuangalia kitu kingine ambacho kiliingia katika machafuko matupu.

Halafu, yanipasa kumwangalia. Atakosa kupiga hatua kwa utaratibu wa hilo Neno nisipomwangalia, wakati anapopita, kama atanikaribia. Labda itakuwa wakati wakati wangu utakapokwisha (mnaona?), nitakapomaliza mwendo, ama cho chote kile.

Yampasa amwangalie, la sivyo atakosa kupiga hatua taratibu wakati anapopita. Lakini kisha anasema labda itakuwa ni wakati wangu, nitakapomaliza mwendo, wakati sipo hapa, Wanaweza kukosa kupiga hatua taratibu kwa kutoyaelekeza macho yao kwake.

Alikuwa akimwonya BIBI-ARUSI waziwazi, Hamna budi kuyaelekeza macho yenu kwenye Sauti ya Mungu iliyo kwenye kanda. Hiyo ndiyo njia iliyoandaliwa na Mungu ya siku hii. Hiyo ndiyo Sauti itakayomunganisha na kumkamilisha Bibi-Arusi. Ukiyaondoa macho na masikio yako kwenye Sauti, Utatoka mstarini na kuingia katika machafuko matupu.

Kila Ujumbe unakuwa wazi zaidi na zaidi. Ni Mungu aliye mkuu Akifunuliwa mbele zetu, akimlisha Bibi-Arusi Wake Mana Iliyofichwa ndiyo tu tunayoweza kula. Ni nono sana kwa wengine wote, bali ni Chakula Kilichofichwa kwa ajili ya Bibi-Arusi.

Ni wakati wa kutoa Shukrani uliyoje Bibi-arusi alionao, akila Neno, akifanyika Bibi-arusi Neno Wake Mkamilifu.

Anasimama peke yake, kama Bwana Arusi, amekataliwa na watu, amedharauliwa na kukataliwa na makanisa. Bibi-arusi yuko hivyo. Ni nini? Ni Kipeo Chake. Mnaona? Ni Neno Yeye analoweza kutendea kazi kwake na kulidhihirisha, likikataliwa.

Njooni muungane nasi Jumapili saa 6:00 MCHANA, saa za Jeffersonville,(ni saa 2 USIKU ya Afrika Mashariki) Wakati Mungu akizungumza kupitia malaika Wake mwenye nguvu, na kutukata na kutuadibisha ili tufanyike Kipeo cha Mungu.

Ndugu Joseph Branham

Ujumbe: 64-0705 Kile Kipeo

Maandiko ya kusoma kabla ya ibada:
Isaya 53:1-12
Malaki 3:6
Mathayo Mt. 24:24
Marko Mt. 9:7
Yohana Mt. 12:24 / 14:19

25-1123 Mungu Aliye Mkuu Akifunuliwa Mbele Zetu

UJUMBE: 64-0629 Mungu Aliye Mkuu Akifunuliwa Mbele Zetu

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Maskani Ya Branham,

Tunakuwa na nyakati tukufu jinsi gani. Neno na Bibi-arusi ni Mmoja na jambo lile lile. Tunaishi nyuma ya pazia katika Uwepo wa Utukufu wa Shekina. Tunamwona Mungu akijificha nyuma ya ngozi katika malaika-mjumbe Wake wa saba. Mungu, kwa mara nyingine tena, akijificha nyuma ya ngozi ya mwanadamu katika kila mmoja wetu. Hakuna swali tena. Hakuna shaka tena, sisi NDIYO wateule Wake, waliochaguliwa tangu zamani, Neno lililofanyika mwili, Bibi-arusi Neno mkamilifu.

Tunapoungana pamoja kutoka kote ulimwenguni, tunaisikiliza Sauti Yake ikinena na kutufunulia Neno Lake kikamilifu ule Ufunuo mkamilifu kwamba Yesu Kristo ni yeye yule jana, leo na hata milele. Dhihirisho la Neno, Elohim, Mungu katika mwili akizungumza na Bibi-arusi Wake. Mungu katika mwili akiishi na kukaa ndani ya kila mmoja wetu. Mpango wa mwisho wa Mungu sasa unadhihirishwa kikamilifu na kuonyeshwa ndani ya kila mmoja wetu.

Tunayofuraha kwelikweli na tunamshukuru Bwana sisi kuitwa wa kipekee na nati zenye hesi za mwonekano wa ajabu. Lakini tunajua yule tuliyeingizwa kwake, na sisi ni nani: Bibi-arusi wa Mungu aliyetiwa Hesi kwa Kanda; Nayo inatuvuta Kwake Yeye Mwenyewe, ikizidi kukaza zaidi na zaidi tunapokuwa MMOJA PAMOJA NAYE, Yesu Kristo yeye yule jana, leo, na hata milele.

Tumepenya katika pazia na kuingia katika Nguzo ya Moto nasi tumetoka na baraka za Mungu! Watu hawawezi kuliona. Hawawezi kulielewa. Lakini kwetu sisi, liko wazi kabisa, kwa sababu tuko katika Roho yule yule na Mtunzi wetu na Kiongozi wetu. Ni Sauti ya Mungu iliyo kwenye Kanda ndiyo inayomwongoza Bibi-arusi Wake.

Tunaishi kwa Mkate wa Wonyesho, Mana inayopewa tu watu waliotengwa. Ndicho Kitu pekee tunachoweza kula. Ndicho kitu pekee tunachoruhusiwa kula. Nacho ni kwa ajili tu ya watu wale ambao wameruhusiwa, waliochaguliwa kimbele na wanaojua hicho nini.

Mimi ninapenda tu kumsikia Yeye akituambia SISI NI NANI:

Yeye aliyeshuka katika siku ya Pentekoste ndiye Roho Mtakatifu yule anayedhihirishwa siku hizi, toka utukufu, hata utukufu, hata utukufu, na kurudia ile mbegu yake asili kwa Ubatizo wa Roho Mtakatifu, pamoja na ishara zile zile, ajabu zile zile ubatizo ule ule, watu wa aina ile ile wakitenda vile vile, wakiwa na uweza ule ule, mwamsho ule ule. Ni kutoka utukufu hata utukufu.

Tumerudi kwenye Mbegu asili pamoja na ubatizo wa Roho Mtakatifu. Ishara zile zile, maajabu yale yale, ubatizo ule ule, watu wa aina ile ile, tukitenda vile vile, kwa uweza ule ule, mwamsho ule ule.

SISI NDIYO BIBI-ARUSI NENO WAKE MKAMILIFU WA KANDA, ALIYEREJESHWA KIKAMILIFU!

Tunashinda. Tunabaki. Tunasimama. Tupo kwenye Neno Lake safi ambalo limehifadhiwa kwa ajili ya Bibi-arusi Wake. Linatukamilisha siku baada ya siku. IMANI yetu imefikia viwango vipya tukijua SISI NI NANI, nayo:

Haikanushiki, Haijadiliki na zaidi ya yote, HAINA MASHARTI.

Je, unataka kuwa mwenye furaha zaidi kuliko ulivyowahi kuwa?
Je, unataka kuridhika 1000% kwamba kile unachokisikia ni Bwana Asema Hivi? Je, unataka kukamilishwa na Neno la Mungu?

Basi ninakualika uje uungane nasi, Maskani ya Branham, Jumapili hii saa 6:00 MCHANA, saa za Jeffersonville, (ni saa 2 USIKU ya Afrika Mashariki) tunapoisikia Sauti ya Mungu ikituambia Maneno ya Uzima wa Milele: Mungu Aliye Mkuu Akifunuliwa Mbele Zetu 64-0629.

Ndugu Joseph Branham

25-1116 Kristo Aliyetambulishwa Katika Nyakati Zote

UJUMBE: 64-0617 Kristo Aliyetambulishwa Katika Nyakati Zote

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Neno La Mungu Lililo Hai,

Miaka hii yote nimelificha moyoni mwangu, nikimficha Kristo, Nguzo ile ile ya Moto ikilifasiri Neno, kama ilivyoahidiwa.

Najua hili litasikika kama la kipuuzi kwa watu wengi, lakini ikiwa tu utamvumilia malaika-mjumbe wa Mungu kwa dakika chache, na kumwomba Mungu Ufunuo zaidi, naamini kwamba yeye, kwa msaada wa Mungu na kwa Neno Lake, na kulingana na Neno Lake, atamleta Yeye hapa mbele yako. Mungu, akijifunua na kujidhihirisha Mwenyewe, akilifasiri na kulifunua Neno Lake.

Ni uamsho ulioje ambao umekuwa ukitendeka mwezi huu uliopita ndani ya Bibi-arusi wa Yesu Kristo. Mungu, akijifunua Mwenyewe zaidi ya wakati wowote ule, akizungumza na Kipenzi Chake, akifanya mapenzi Naye, akimhakikishia, Sisi ni Mmoja na Yeye.

Hakuna kusitasita, hakuna kutokuwa na uhakika, hakuna kushuku, hakuna shaka hata chembe; Mungu ametufunulia: Sauti ya Mungu inayozungumza kwenye kanda ndio NJIA YA MUNGU ILIYOANDALIWA NA ILIYOKAMILIFU KWA BIBI-ARUSI WAKE LEO.

Aliiandaa njia hii ili Tusije kamwe tukalazimika hilo kuwekewa chujio, kufafanuliwa, kuelezewa, wala kushikwa-shikwa na mikono ya watu kwa njia yoyote; kuisikiliza tu Sauti Safi ya Mungu ikizungumza mdomo kwa sikio na kila mmoja wetu.

Yeye alijua siku hii ilikuwa inakuja. Alijua Bibi-arusi Wake angeweza kula tu hiyo Mana iliyofichwa, Chakula Chake cha Kondoo. Hatungetaka kusikia chochote ila Sauti ya Mungu kutoka kwa Mungu Mwenyewe.

Tumevunja tukapitia kwenye pazia hilo nasi tumeingia katika Utukufu wa Shekina. Ulimwengu hauwezi kuliona. Nabii wetu huenda asiyatamke maneno yake ipasavyo. Huenda asivalie ipasavyo. Huenda asivikwe mavazi ya kikasisi. Lakini nyuma ya ngozi hiyo ya kibinadamu, mle ndani mna ule Utukufu wa Shekina. Mle ndani mna nguvu. Mle ndani mna Neno. Mle ndani mna Mkate wa Wonyesho. Mle ndani mna Utukufu wa Shekina, ambao ndiyo Nuru inayomwivisha Bibi-arusi.

Na mpaka utakapokuja nyuma ya hiyo ngozi ya pomboo, mpaka utakapotoka nyuma ya ngozi yako ya kale, mawazo yako ya kale, kanuni zako za imani za kale, na uingie katika Uwepo wa Mungu; ndipo Neno linakuwa hali halisi iliyo hai kwako, ndipo umeinuka katika Utukufu wa Shekina, ndipo Biblia inakuwa ni Kitabu Kipya, ndipo Yesu Kristo ni yeye yule jana, leo, na hata milele. Unaishi katika Uwepo Wake, ukila mkate wa wonyesho ambao unatolewa tu siku hiyo kwa waaminio, makuhani pekee. “Na sisi ni makuhani, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kipekee, tukimtolea Mungu dhabihu za kiroho.” Lakini huna budi kuingia, huko nyuma ya pazia, upate kumwona Mungu aliyefunuliwa. Na Mungu anafunuliwa, hilo ni Neno Lake lililodhihirishwa.

Sisi ni wa kipekee kwa ulimwengu, lakini tumeridhika kujua Skrubu yetu ni nani na tunajivunia sisi kuwa nati Zake za kanda, tuliyotiwa hesi kwa Neno Lake, kwani linatuvuta Kwake.

Kama hujaingizwa kwenye kanda, wewe si kitu ila lundo la vitu shaghalabaghala!!!

Sasa, angalieni sasa, Mungu! Yesu alisema ya kwamba, “Wale waliojiliwa na Neno, waliitwa ‘miungu,’” hao walikuwa ni manabii. Sasa, si kwamba mtu huyo mwenyewe alikuwa ni Mungu, si zaidi ya vile mwili wa Yesu Kristo ulivyokuwa ni Mungu. Yeye alikuwa ni mwanadamu, Naye Mungu alikuwa amefunikwa nyuma yake.

Mungu, siku moja alifunikwa nyuma ya ngozi za pomboo. Mungu, siku moja alifunikwa katika mwili wa mwanadamu aitwaye Melkizedeki. Mungu, alifunikwa katika mwili wa mwanadamu aitwaye Yesu. Mungu, alifunikwa katika mwili wa mwanadamu aitwaye William Marrion Branham. Mungu, amefunikwa katika mwili wa mwanadamu aitwaye BIBI-ARUSI WAKE.

Ni muhimu sana kukumbuka, lakini walio wengi wanashindwa na wanatafuta kitu kingine. Jambo la mwisho ambalo Ibrahimu aliona, jambo la mwisho kutukia kabla ya moto kushuka na kuuhukumu ulimwengu wa Mataifa, kabla ya yule mwana aliyeahidiwa kutokea, jambo la mwisho ambalo kanisa la Kikristo litaliona mpaka kule kuonekana kwa Yesu Kristo ni Melkizedeki, Mungu aliyedhihirishwa katika mwili, akilifunua Neno Lake kwa Bibi-arusi Wake.

Hakuna kitu kingine kitakachokuja. Hakuna kitu kingine kilichoahidiwa katika Neno Lake. Hakuna mtu, wala kundi la watu watakaokuja kumkamilisha Bibi-arusi.

La! Wanataka kuja humu kanisani kwa ajili ya kukamilishwa. Ona? Ili sisi—sisi tupate ushirika sisi kwa sisi hapa kanisani, lakini kukamilishwa huja kati yetu na Mungu. Damu ya Kristo ndiyo inayotukamilisha katika Roho Mtakatifu.

Ujumbe huu, Sauti Hii, Neno la Mungu lililothibitishwa, linamkamilisha Bibi-arusi wa Yesu Kristo.

Ninawaalika kila mmoja wenu mje muisikilize pamoja nasi Sauti ya Mungu inapomkamilisha Bibi-arusi Wake Jumapili hii saa 06:00 MCHANA, saa za Jeffersonville,(ni saa 2 USIKU ya Afrika Mashariki) tunaposikia: 64-0617 “Kristo Aliyetambulishwa Katika Nyakati Zote”.

Ndugu. Joseph Branham

Maandiko ya kusoma kabla ya Ujumbe:
Kumbukumbu la Torati 18:15
Zekaria 14:6
Malaki 3: 1-6
Luka Mtakatifu 17: 28-30
Yohana Mtakatifu 1:1 / 4:1-30 / 8: 57-58 / 10:32-39
Waebrania 1:1 / 4:12 / 13:8
Ufunuo 22:19