Category Archives: Uncategorized

25-0126 Ufunuo, Mlango Wa Tano Sehemu Ya II

UJUMBE: 61-0618 Ufunuo, Mlango Wa Tano Sehemu Ya II

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wapumzikao,

Hakika haya ni Majira ya baridi yaliyo bora maishani mwetu. Kuja kwa Bwana kumekaribia. Tumetiwa muhuri na Roho Mtakatifu; Muhuri wa kibali cha Mungu kwamba kila kitu alichokifia Kristo ni mali yetu. 

Sasa tunayo arabuni ya urithi wetu, Roho Mtakatifu. Ni hakikisho, yale malipo ya kwanza, ya kwamba tumepokelewa katika Kristo. Tunapumzika katika ahadi za Mungu, tukilala katika joto la Mwangaza Wake wa Jua; Neno Lake lililothibitishwa, tukiisikiliza Sauti Yake.  

Ni arabuni ya wokovu wetu. Hatuna wasiwasi kama tunaenda kule ama hatuendi, TUNAENDA! Tunalijuaje hilo? Mungu alisema hivyo! Mungu aliliahidi nasi tunayo arabuni. Tayari tumeipokea na Kristo ametukubali.

Hakuna njia ya kuliondokea…kwa kweli, tupo hapo! Yote itupasayo kufanya ni kungojea tu; Yeye anafanya kazi ya Mkombozi wa Jamaa wa Karibu sasa hivi. Tunayo Arabuni yake sasa hivi. Tunangojea tu wakati ambapo Yeye atakaporudi kutuchukua. Kisha, katika dakika moja, katika kufumba na kufumbua jicho, sote tutakuwa tumekwenda kwenye Karamu ya Arusi.

Kuwazia tu yale yote yaliyo mbele yetu. Akili zetu haziwezi kuyaingiza yote ndani. Siku baada ya siku Yeye analifunua zaidi Neno Lake, akihakikisha kwamba ahadi hizi kuu ni zetu.

Ulimwengu Unaporomoka; mioto, matetemeko ya ardhi, na machafuko kila mahali, lakini wao wanaamini kuwa wanaye mwokozi mpya ambaye atauokoa ulimwengu, na kuwaletea wakati wao wa heri na furaha kuu. Tayari sisi tumekwishampokea Mwokozi wetu nasi tumekuwa tukiishi katika Wakati wetu wa Heri na Furaha Kuu. 

Sasa Yeye anatutayarisha kwa Ufunuo hata na zaidi wakati tunapoingia katika mlango wa 5 wa Ufunuo. Anaandaa tukio hapa kwa ajili ya kufunguliwa kwa ile Mihuri Saba. Kama tu vile alivyofanya katika mlango wa 1 wa Ufunuo, akiifungua njia kwa ajili ya Nyakati Saba za Kanisa.

Je! Majira mengine yaliyosalia ya baridi yatakuwaje kwa Bibi-arusi? Hebu tuangalie muhtasari mdogo:

Sasa, sina wakati. Nimeiandika, muktadha fulani juu yake hapa, bali mkutano wetu ujao kabla hatujaliingilia hili…Labda nitakapotoka kwenye likizo yangu ama wakati mwingine, ninataka kuyachukua haya majuma sabini ya Danieli na kuyafunganisha mumu humu, na kuonyesha mahali yanapolipeleka kwenye Yubile ya Pentekoste, na kuyarejesha moja kwa moja pamoja na vile ninii saba…hiyo mihuri saba itakayofunguliwa hapa kabla tu hatujaenda, na kuonyesha kwamba ni wakati wa mwisho, hii…

Ni wakati wa ajabu jinsi gani Bwana aliomwekea Bibi-arusi Wake. Akijifunua Mwenyewe katika Neno Lake kwetu zaidi ya hapo awali. Akitutia moyo kwamba sisi ndio wateule Wake anaowajia Yeye. Akituambia tuko katika mapenzi Yake Makamilifu kwa kukaa na Sauti Yake, na Neno Lake.

Tunafanya nini? Si hata jambo moja, tunapumzika tu! Tunangojea! Hakuna kutenda kazi tena, hakuna masumbuko tena, TUNAPUMZIKA KWENYE HILO!

Njoo upumzike pamoja nasi Jumapili hii saa 06:00 SITA MCHANA, saa za Jeffersonville, (Ni saa 2:00 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki) tunapoisikia Sauti ya Mungu ILIYOTHIBITISHWA ikituletea Ujumbe: 

61-0618 – “Ufunuo, Mlango wa Tano Sehemu ya II”.

Ndugu. Joseph Branham

25-0119 Ufunuo, Mlango Wa Tano Sehemu Ya I

UJUMBE: 61-0611 Ufunuo, Mlango Wa Tano Sehemu Ya I

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wana Wenye Mamlaka, 

Ni Majira ya baridi ya ajabu jinsi gani tuliyonayo Roho Mtakatifu anavyoangazia Neno Lake kuliko hapo awali. Mambo ambayo labda tumeyasikia, kuyasoma na kujifunza maisha yetu yote sasa yanawekwa wazi na kufunuliwa zaidi ya hapo awali. 

Mwanadamu amengojea kwa maelfu ya miaka kuifikia siku hii hasa. Wote walitamani na kuomba ili kusikia na kuyaona mambo tunayoyaona na kusikia.  Hata manabii wa kale waliitamani siku hii.  Jinsi gani walivyotaka kuona kule kutimizwa na kuja kwa Bwana.

Hata wanafunzi wa Yesu, Petro, Yakobo, na Yohana, watu waliotembea na kuzungumza Naye, walitamani kuona na kusikia yote yaliyokuwa yamefichwa.  Waliomba lifunuliwe na kudhihirishwa katika siku yao, katika wakati wao.

Kote katika zile Nyakati Saba za Kanisa, kila mjumbe, Paulo, Martin, na Luther, walitaka kuzijua zile siri zote zilizokuwa zimefichwa. Haja yao ilikuwa ni kuona kule kutimizwa kwa Neno kukitendeka kipindi wawapo hai. Walitaka kuona kule kuja kwa Bwana.

Mungu alikuwa na mpango. Mungu alikuwa na wakati. Mungu alikuwa na watu aliokuwa akiwangojea…SISI. Katika nyakati zote, wote walishindwa.  Bali Yeye alijua, kwa kujua Kwake tangu zamani, kungekuwako na watu: Bibi-arusi wa Neno Lake tukufu na kamilifu. WAO HAWANGEMWANGUSHA YEYE. Hawangepatana HATA KWA NENO MOJA. Wangekuwa Bibi-arusi Neno Wake aliye bikira safi.

Sasa huu ndio wakati. Sasa haya ndio majira. Sisi ndio wale wateule ambao Yeye amewangojea tangu Adamu alipoanguka na kupoteza haki yake. SISI NI BIBI-ARUSI WAKE.

Mungu alimwonyesha Yohana kuonekana kimbele kwa yote ambayo yangetukia, lakini hakujua maana zote. Naye alipoitwa juu, aliona katika mkono wa kuume wake yeye aliyeketi juu ya kile kiti cha enzi kitabu kilichoandikwa ndani, kilichotiwa muhuri saba, lakini hapakuwa na mtu ye yote aliyestahili kukifungua hicho kitabu.

Yohana alipiga kelele na kulia sana kwani yote yalikuwa yamepotea, hakukuwepo na tumaini. Lakini Bwana asifiwe, mmoja wa wale wazee akamwambia, “Usilie, kwa maana tazama, Simba wa kabila la Yuda, Shina la Daudi, Yeye ameshinda kukifungua kile kitabu, na kuifungua muhuri zake saba”.

Huo ulikuwa ndio wakati. Hayo yalikuwa ndio majira. Huyo alikuwa ndiye mtu ambaye Mungu alikuwa amemchagua kuyaandika yote aliyoyaona. Lakini bado, Haikujulikana maana Yake yote. 

Mungu alikuwa akingojea na kungojea chombo Chake kiteule, malaika-mjumbe Wake wa saba, aje duniani, ili Yeye aweze kuitumia sauti yake kuwa Sauti Yake, kwa Bibi-arusi Wake. Yeye alitaka kunena mdomo kwa sikio ili KUSIWEKO KUTOELEWA. Yeye Mwenyewe, alitaka kunena na kuzifunua siri Zake zote kwa Bibi-arusi Wake Kipenzi, mpendwa, aliyechaguliwa tangu awali, mkamilifu…SISI!!

Jinsi ambavyo Yeye ametamani kutuambia mambo haya yote ya ajabu. Kama vile mwanamume anavyomwambia mke wake kwamba anampenda mara kwa mara, na yeye hachoki kulisikia hilo, Yeye anapenda kutuambia mara kwa mara kwamba anatupenda, alituchagua, alitungojea, na sasa anakuja kutuchukua.

Yeye alijua jinsi gani tungependa kumsikia Yeye Akilisema tena na tena, kwa hiyo akaifanya Sauti Yake irekodiwe, hivyo Bibi-arusi Wake angeweza ‘Kubonyeza Play’ siku nzima, kila siku, na kulisikia Neno Lake likiijaza mioyo yao. 

Bibi-arusi Wake kipenzi amejiweka tayari kwa kujilisha Neno Lake. Hatutasikiliza kitu kingine cho chote, Sauti Yake tu. Tunaweza tu kutumia Neno Lake Safi lililotolewa.

Tuko chini ya matarajio makubwa. Tunalihisi hilo ndani ya nafsi zetu. Yeye anakuja. Tunausikia muziki wa harusi ukicheza. Bibi-arusi anajitayarisha kutembea kwenye marefu ya ukumbi. Kila mtu asimame, Bibi-arusi anakuja kuungana na Bwana Arusi wake. Yote yamekwisha tayarishwa. Wakati umefika.

Yeye anatupenda zaidi ya yeyote yule. Tunampenda zaidi ya yeyote yule. Tunakwenda kuwa Mmoja na Yeye, na wale wote tuwapendao, milele. 

Unaalikwa kuja kujiweka mwenyewe tayari kwa ajili ya harusi pamoja nasi Jumapili saa 06:00 SITA MCHANA, saa za Jeffersonville,(Ni saa 2 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki) tunapoisikia Sauti ya Mungu ikifunua Ufunuo, Mlango Wa Tano Sehemu ya I   61-0611.

Ndugu. Joseph Branham

25-0112 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu Ya III

UJUMBE: 61-0108 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu Ya III

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wa Milele,

Ni wakati wa sisi kuvua kofia yetu ya vita na mvae mawazo yenu ya kiroho, maana Mungu anajitayarisha kumpa Bibi-arusi Wake Ufunuo zaidi wa Neno Lake.

Yeye atakuwa akitufunulia siri zote za wakati uliopita. Atatuambia yale yatakayotukia wakati ujao. Yale ambayo wengine wote katika Biblia waliyoyaona au kusikia, Yeye atafunua kila jambo dogo la Neno Lake na maana Yake kwetu.

Tutasikia na kuelewa maana ya alama za Biblia: Viumbe Hai, Bahari ya Kioo, Simba, Ndama, Mwanadamu, Tai, Kiti cha Rehema, Walinzi, Wazee, Sauti, Therion, Zoon.

Tutasikia na kuelewa yote kuhusu walinzi wa Agano la Kale. Yuda: Mlinzi wa Mashariki; Efraimu: Mlinzi wa Magharibi; Rubeni: Mlinzi wa Kusini; na Dani: Mlinzi wa Kaskazini.

Hakuna kitu kingaliweza kuja popote karibu na hicho kiti cha rehema pasipo kuyapitia makabila hayo. Simba, akili ya mwanadamu; Maksai: farasi mtenda-kazi; Tai: Wepesi wake.

Jinsi Mbingu, nchi, katikati, na kote kote huku, walikuwa ni walinzi. Na juu yake ilikuwa ile Nguzo ya Moto. Hakuna kitu kilichogusa kiti hicho cha rehema pasipo kuyapitia makabila hayo.

Sasa kuna walinzi wa Agano Jipya: Mathayo, Marko, Luka na Yohana, wakienda mbele moja kwa moja. Lango la mashariki limelindwa na simba, lango la kaskazini limelindwa na tai arukaye, Yohana, yule mwinjilisti. Halafu tabibu upande huu, Luka, mwanadamu.

Zile Injili nne zinalinda Baraka za Kipentekoste pamoja na kila Andiko kuunga mkono yale hasa waliyosema. Na sasa Matendo ya mitume yanathibitisha leo hii pamoja na zile Injili nne ya kwamba Yesu Kristo ni yeye yule jana, leo, na hata milele.

Wakati mpakwa mafuta wa kweli wa Mungu anaponena, ni Sauti ya Mungu! Tunataka tu kupaza sauti, “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu kwa Bwana!”

Hakuna njia ya kumwacha Huyo. Kwa kweli, Hatuwezi kumwacha, kwa kuwa Yeye hatatuacha. Tumetiwa muhuri hata Siku ya ukombozi wetu. Hakuna cha usoni, hakuna cha wakati uliopo, hatari, njaa, kiu, mauti, wala CHOCHOTE KILE, kinachoweza kututenganisha na upendo wa Mungu ulio ndani ya Kristo.

Kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu majina yetu yaliwekwa kwenye Kitabu cha Uzima cha Mwana-Kondoo ili kuiona Nuru HII, kuipokea Sauti Hii, kuuamini Ujumbe Huu, kumpokea Roho Mtakatifu wa wakati wetu na kutembea ndani Yake. Wakati Mwana-Kondoo alipochinjwa, MAJINA YETU yaliwekwa kwenye Kitabu wakati ule ule Jina la Mwana-Kondoo lilipowekwa mle. UTUKUFU!!

Hivyo, hakuna kinachoweza kututenganisha na Ujumbe huu. Hakuna kinachoweza kututenganisha na Sauti hiyo. Hakuna kinachoweza kuuondoa Ufunuo wa Neno Hili kutoka kwetu. Ni wetu. Mungu alituita na akatuchagua na kutuchagua tangu awali. Kila kitu ni chetu, ni yetu.

Kuna njia moja tu ya kuyapata haya yote. Ni lazima uoshwe kwa maji ya Neno. Huna budi kulisikia Neno kabla hujaingia Mle. Na kuna njia moja tu unayoweza kumkaribia Mungu, hiyo ni kwa Imani. Na Imani huja kwa kusikia, kusikia Neno la Mungu, ambalo linaakisiwa kutoka Patakatifu pa Patakatifu ndani ya mjumbe wa wakati.

Kwa hiyo, hapa, malaika wa wakati wa kanisa anaakisi kuingia kwenye maji hayo kwamba Jamaa huyu ni nani hapa, akiakisi rehema Zake, Maneno Yake, hukumu Yake, Jina Lake. Yote yanaakisiwa humu ndani ambako unatenganishwa kwa kuliamini. Unalipata?

Usiache kuzisikiliza kanda, wewe dumu nalo tu. Lichunguze kwa Neno na uone kama ni kweli. Ni Njia iliyoandaliwa na Mungu kwa ajili ya siku hii.

Njoo uungane nasi Majira haya ya baridi wakati tunapoungana pamoja kutoka kote ulimwenguni na kuisikia Sauti ya Mungu ikilifunua Neno Lake kwa Bibi-arusi Wake kuliko hapo awali. Hakuna upako mkuu kuliko kubonyeza play na kusikiliza Sauti Yake.

Kutoka katika kilindi cha moyo wangu, Naweza kusema: Nina furaha sana naweza kusema Mimi ni Mmoja Wao pamoja na kila mmoja wenu.

Ndugu. Joseph Branham

Ujumbe: 61-0108 – “Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu ya III”

Muda: saa 6:00 SITA MCHANA Saa za Jeffersonville ( ni Saa 2:00 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki )

25-0105 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu Ya II

UJUMBE: 61-0101 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu Ya II

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi-arusi wa Kanisa la Nyumbani,

Hebu sote tukusanyike pamoja na kuusikia Ujumbe,   61-0101 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu ya II Jumapili hii saa 06:00 SITA MCHANA, saa za Jeffersonville.(Ni saa 2 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki)

Ndugu Joseph Branham

24-1231 Lile Shindano Na Ushirika

UJUMBE: 62-1231 Lile Shindano

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi arusi,

Natumai kila mmoja wenu alikuwa na Krismasi nzuri pamoja na marafiki na familia yako. Ninayo shukurani jinsi gani leo kujua ya kwamba Bwana wetu Yesu hajakwama horini kama ulimwengu unavyomwona Yeye leo, lakini yu hai na Yuko katikati ya Bibi-arusi Wake, akijifunua Mwenyewe kupitia Sauti Yake kuliko hapo awali, BWANA ASIFIWE.

Kama nilivyokwishatangaza, ningependa tuwe na Ushirika kwa mara nyingine tena katika nyumba zetu/makanisa yetu katika mkesha wa Mwaka Mpya, tarehe 31 Desemba. Kwa wale wanaotaka kushiriki, tutasikiliza Ujumbe,  62-1231 Lile Shindano, na kisha kuingia moja kwa moja kwenye ibada ya Ushirika, ambayo Ndugu Branham anaitambulisha wakati wa kuhitimisha Ujumbe.

Kwa waamini walio eneo hili, tutaanza kanda saa 1:00 MOJA JIONI. Hata hivyo, kwa wale walio katika maeneo ya majira tofauti, tafadhali uanzeni Ujumbe kwa wakati unaofaa kwenu. Baada ya Ndugu Branham kuleta Ujumbe wake wa Mkesha wa Mwaka Mpya, tutasimamisha kanda mwishoni mwa aya ya 59, na kuwa na takriban dakika 10 za muziki wa piano wakati tunapokula Meza ya Bwana. Kisha tutaendeleza tena kanda Ndugu Branham anapofunga ibada. Kwenye kanda hii, yeye anaiacha sehemu ya ibada ya Kutawadhana miguu, ambayo na sisi pia tutaiacha.

Maagizo ya jinsi ya kupata divai, na jinsi ya kuoka mkate wa Ushirika yanaweza kupatikana katika anuani zilizo hapa chini. Unaweza kucheza au kupakua sauti kutoka kwenye tovuti, au unaweza tu kuicheza ibada kwenye Redio ya Sauti kwenye programu ya Lifeline (ambayo itachezwa kwa Kiingereza saa 1:00 JIONI saa za Jeffersonville.)

Wakati tunapoukaribia mwaka mwingine wa huduma kwa Bwana wetu, hebu na tuonyeshe upendo wetu Kwake kwa kuisikia kwanza Sauti Yake, na kisha tushiriki Meza Yake. Utakuwa wakati wa utukufu na mtakatifu jinsi gani wakati tunapoyaweka upya maisha yetu kwa ajili ya Huduma Yake.

Mungu awabariki,

Ndugu Joseph

24-1229 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu Ya I

UJUMBE: 60-1231 Ufunuo, Mlango Wa Nne Sehemu Ya I

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Watakatifu Waliovikwa Mavazi Meupe,

Wakati tunapoisikia Sauti ya Mungu ikisema nasi, jambo fulani hutokea ndani kabisa ya nafsi zetu. Utu wetu wote unabadilishwa na ulimwengu unaotuzunguka unaonekana kufifia.

Mtu anawezaje kueleza kile kinachotendeka katika mioyo yetu, akili zetu, na nafsi zetu, wakati Sauti ya Mungu inapofunua Neno Lake kwa kila Ujumbe tunaousikia?

Kama vile nabii wetu, tunahisi tumenyakuliwa hadi kwenye mbingu ya tatu nazo nafsi zetu zinaonekana kuuacha mwili huu upatikanao na mauti. Hakuna maneno ya kueleza kile tunachojisikia Mungu anapotufunulia Neno Lake kuliko hapo awali.

Yohana aliwekwa kwenye kisiwa cha Patmo naye akaombwa aandike kile alichokiona na kukiweka kwenye kitabu kiitwacho Ufunuo, ili kiende katika nyakati zote. Siri hizo zilikuwa zimefichwa hadi zilipofunuliwa kwetu kupitia malaika-mjumbe Wake wa 7 aliyemchagua.

Kisha Yohana akasikia Sauti iyo hiyo juu yake naye akanyakuliwa hadi katika mbingu ya tatu. Sauti hiyo ilimwonyesha nyakati za kanisa, kuja kwa Wayahudi, kumwagwa kwa yale mapigo, Kunyakuliwa, Kuja mara ya pili, Utawala wa Miaka Elfu, na Makazi ya Milele ya waliookolewa Wake. Alimchukua na kumwonyesha Yohana kitu hicho chote kikifanyiwa mazoezi kama Yeye alivyosema angefanya.

Lakini Yohana alimwona nani wakati alipoyaona yale mazoezi? Hakuna kweli aliyejua hadi leo hii.

Kitu cha kwanza alichoona katika kule Kuja kilikuwa ni Musa, aliyewawakilisha watakatifu waliokufa ambao wangefufuliwa; nyakati zote sita walizolala. Lakini si Musa tu peke yake aliyekuwa amesimama pale, bali Eliya alikuwa pale pia.

Yule Eliya aliyekuwa amesimama alikuwa ni nani?

Bali Eliya alikuwako; yule mjumbe wa siku ya mwisho, pamoja na kundi lake, la waliobadilishwa, Walionyakuliwa.

UTUKUFU…HALELUYA… ni nani ambaye Yohana alimuona akiwa amesimama pale?

Si mwingine ila malaika-mjumbe wa 7 wa Mungu, William Marrion Branham, pamoja na KUNDI LAKE LA WALIOBADILISHWA, WALIONYAKULIWA…KILA MMOJA WETU!!

Eliya aliwakilisha watakatifu waliokufa …Ninamaanisha Musa, na kufufuliwa. Eliya aliwakilisha kundi lililohamishwa. Kumbukeni, Musa alikuwa wa kwanza, na kisha Eliya. Eliya alikuwa awe ndiye mjumbe wa siku za mwisho, ili kwa yeye na kundi lake ungekuja ufufuo…ungekuja ninii…vema, ungekuja Unyakuo, namaanisha. Musa alileta ufufuo na Eliya akaleta kundi Lililonyakuliwa. Na, hapo, wote wawili waliwakilishwa papo hapo.

Nena kuhusu kufichua, kufunua, na Ufunuo.

Hii hapa! Tunaye moja kwa moja pamoja nasi sasa, Roho Mtakatifu, Yesu Kristo, yeye yule jana, leo, na hata milele. Wewe ni…Anawahubiria, anawafundisha, anajaribu kuwafanya muone yaliyo mema na mabaya. Ni Roho Mtakatifu Mwenyewe akinena kupitia midomo ya wanadamu, akifanya kazi miongoni mwa wanadamu, akijaribu kuonyesha rehema na neema.

Sisi ndio wale Watakatifu Waliovikwa Mavazi Meupe ambao malaika Wake aliwaona wakija kutoka kote ulimwenguni kula Mkate wa Uzima. Tumeposwa na kuolewa Naye nasi tumehisi busu Lake la posa mioyoni mwetu. Tumetoa kiapo Kwake, na kwa Sauti Yake tu. Hatuna, nasi hatutajitia unajisi kwa sauti nyingine yoyote.

Bibi-arusi anajitayarisha kupanda juu kama Yohana alivyofanya; kuingia Uweponi mwa Mungu. Tutatwaliwa juu kwenye Unyakuo wa Kanisa. Jinsi hilo linavyozizungusha nafsi zetu!

Ni kipi kifuatacho Yeye anachoenda kutufunulia?

Hukumu; jiwe la akiki, na kile linachowakilisha; kazi yake. Yaspi, na mawe yote mbalimbali. Yeye atayachukua haya yote kote kupitia kwa Ezekieli, arudi kwenye Mwanzo, arejee kwenye Ufunuo, aje katikati ya Biblia, ayafungamanishe pamoja; mawe haya yote mbalimbali na rangi.

Ni Roho Mtakatifu yeye yule, Mungu yeye yule, akionyesha ishara zile zile, maajabu yale yale, akifanya jambo lile lile kama Yeye alivyoahidi. Ni Bibi-arusi wa Yesu Kristo akijiweka mwenyewe tayari kwa kuisikia Sauti Yake.

Tunawakaribisha kuungana nasi tunapoingia katika ulimwengu wa roho saa 6:00 SITA MCHANA, saa za Jeffersonville (Ni saa 2:00 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki), kumsikia Eliya, mjumbe wa Mungu kwa wakati huu wa mwisho, akifunua siri ambazo zimefichwa katika nyakati zote.

Ndugu. Joseph Branham

Ujumbe: 60-1231 Ufunuo, Mlango wa Nne Sehemu ya I

. Tafadhali ukumbukeni Ujumbe wetu wa Mwaka Mpya, Jumanne usiku: Lile Shindano 62-1231. Hakuna njia bora ya kuuanza Mwaka Mpya.

24-1222 Zawadi Ya Mungu Iliyofungwa

UJUMBE: 60-1225 Zawadi Ya Mungu Iliyofungwa

PDF

BranhamTabernacle.org

Mpendwa Bibi. JEZU,

Ee Mwana-Kondoo wa Mungu, Wewe ndiwe Zawadi iliyo kuu ya Mungu iliyofungwa kwa ulimwengu. Umetupa Zawadi iliyo kuu kuliko zote iliyowahi kutolewa, Wewe Mwenyewe. Kabla haujaumba nyota ya kwanza, kabla haujaumba dunia, mwezi, mfumo wa jua, ulitujua sisi na kutuchagua tuwe Bibi-arusi Wako.

Ulipotuona wakati huo, ulitupenda. Tulikuwa nyama ya nyama Yako, mfupa wa mfupa Wako; tulikuwa sehemu Yako. Jinsi Ulivyotupenda na kutaka kushirikiana nasi. Ulitaka kuushiriki Uzima Wako wa Milele nasi. Tulijua basi, tungekuwa Bibi JEZU Wako.

Uliona tungeshindwa, kwa hivyo Wewe ulilazimika kuiandaa njia ya kuturudisha sisi. Tulikuwa tumepotea na bila tumaini. Kulikuwa na njia moja tu, Ilibidi Wewe ufanyike “Uumbaji Mpya”. Ilibidi Mungu na mwanadamu wawe Mmoja. Ilibidi Wewe ufanyike sisi, ili sisi tuweze kuwa Wewe. Hivyo, Ukauweka mpango Wako mkuu utende kazi maelfu ya miaka iliyopita katika bustani ya Edeni.

Umetamani sana kuwa pamoja nasi, Bibi-arusi Wako wa Neno kamilifu, lakini Wewe ulijua kwanza Ilikubali uturudishe sisi kwenye yale yote yaliyokuwa yamepotea hapo mwanzo. Ulingoja na kungoja na kungoja hadi siku hii kuukamilisha mpango Wako.

Siku hiyo imefika. Lile kundi dogo uliloliona hapo mwanzo liko hapa. Kipenzi chako anayekupenda Wewe na Neno Lako kuliko kitu chochote.

Ilikuwa ni wakati Wako wa kuja na kujidhihirisha Mwenyewe katika mwili wa mwanadamu kama ulivyofanya kwa Ibrahimu, na kama ulivyofanya ulipofanyika Uumbaji mpya. Jinsi Wewe umeisubiri kwa hamu siku hii ili uweze kutufunulia sisi siri Zako zote kuu zilizofichwa tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu.

Unamjivunia sana Bibi-arusi Wako. Jinsi Wewe unavyopenda kumwonyesha Yeye na kumwambia Shetani, “Hata ujaribu kuwafanyia nini, wao hawataondoshwa; hawatapatana kuhusu Neno Langu, Sauti Yangu. Wao ni BIBI-ARUSI Wangu wa NENO KAMILIFU.” Wao ni wakupendeza sana Kwangu. Hebu Watazame tu! Kupitia majaribio na majaribu yao yote, wao wanabaki waaminifu kwa Neno Langu. nitawapa zawadi ya milele. Yote niliyo Mimi, Nawapa wao. TUTAKUWA MMOJA.

Tunachoweza tu kusema ni: “JEZU, TUNAKUPENDA. Jalia tukukaribishe nyumbani mwetu. Hebu na tukupake Wewe mafuta na tuioshe miguu Yako kwa machozi yetu na kuibusu. Hebu na tukuambie jinsi tunavyokupenda Wewe.”

Yote tuliyo, tunakupa wewe JEZU. Hiyo ndiyo zawadi yetu Kwako JEZU. Tunakupenda. Tunakuhimidi. Tunakuabudu.

Ninawaalika kila mmoja wenu aungane nasi Jumapili saa 6:00 SITA MCHANA, saa za Jeffersonville,(Ni saa 2:00 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki) na umkaribishe JEZU nyumbani kwako, kanisani kwako, ndani ya gari lako, popote uwezapo kuwa, na uipokee Zawadi iliyo kuu kuliko zote iliyowahi kutolewa kwa mwanadamu; Mungu Mwenyewe akizungumza na kushirikiana nawe.

Ndugu. Joseph Branham

60-1225 Zawadi ya Mungu Iliyofungwa

TANGAZO MAALUM

Mpendwa Bibi-arusi,

Bwana ameweka moyoni mwangu kuwa na Ujumbe Maalum na Ibada ya Ushirika katika Mkesha wa Mwaka Mpya tena mwaka huu. Ni jambo gani kubwa zaidi tunaloweza kufanya, Enyi marafiki, kuliko kuisikia Sauti ya Mungu ikizungumza nasi, kushiriki Meza ya Bwana, na kuyaweka wakfu tena maisha yetu kwa huduma Yake wakati wa kuukaribisha Mwaka Mpya. Utakuwa wakati mtakatifu jinsi gani kuufungia nje ulimwengu, na kuungana na Bibi-arusi kwa ajili ya huku kukusanyika Maalum katika Neno, tunaposema kutoka mioyoni mwetu, “Bwana, utusamehe makosa yote tuliyofanya mwaka mzima; sasa tunakukaribia Wewe, tukikuomba ikiwa utatushika mkono na kutuongoza mwaka huu ujao. Jalia tukutumikie Wewe zaidi ya tulivyowahi, na kama ni katika Mapenzi Yako ya Kiungu, jalia uwe ndio mwaka wa ule Unyakuo mkuu utakaotukia. Bwana, tunataka tu kwenda Nyumbani kuishi Nawe Milele yote.” Nasubiri kwa hamu kukusanyika kukizunguka Kiti Chake cha Enzi kwa ajili ya ibada hii maalum ya kujiweka wakfu upya, Bwana asifiwe.

Kwa waamini walio katika eneo la Jeffersonville, ningependa kuianza kanda saa 1:00 MOJA JIONI katika saa za eneo letu. Ujumbe kamili na ibada ya Ushirika itakuwa kwenye Redio ya Sauti wakati huo, kama tulivyofanya wakati uliopita. Vifurushi vya divai ya Ushirika vtapatikana Jumatano, tarehe 18 Desemba, kuanzia 7:00 – 11:00 jioni, kwa wewe kuja kuchukua kwenye jengo la YFYC.

Kwa wale ambao wanaishi nje ya eneo la Jeffersonville, tafadhali iweni na ibada hii maalum kwa wakati unaofaa kwenu. Tutakuwa na anuani ya kupakuliwa yenye Ujumbe na Ushirika hivi karibuni.

Tunapokaribia Sikukuu ya Krismasi, nataka nikutakie wewe na familia yako Msimu wa AJABU na SALAMA wa Sikukuu, na KRISmasi Njema, iliyojaa furaha ya Bwana Yesu aliyefufuka…Lile NENO.

Mungu awabariki,

Ndugu Joseph

Chanzo : https://branhamtabernacle.org/en/bt/F6/110067

24-1208 Wakati wa Kanisa La Laodikia

UJUMBE: 60-1211E Wakati wa Kanisa La Laodikia

PDF

BranhamTabernacle.org

Wapendwa Wateule,

Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti Yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja Nami.

Enyi wahudumu, mfungulieni milango yenu malaika wa Mungu kabla hamjachelewa. Irudisheni Sauti ya Mungu kwenye mimbara zenu kwa kuzicheza kanda. Ndiyo Sauti pekee ya Mungu iliyothibitishwa kwa ajili ya siku yetu yenye Maneno ya kutokosea. Ndiyo Sauti pekee yenye Bwana Asema Hivi. Ndiyo Sauti pekee ambayo Bibi-arusi wote wanaweza kusema AMINA kwake.

Huu ndio wakati mkuu wa nyakati zote. Yesu anatupa sifa Yake kwa vile siku za neema Yake zinakwisha. Wakati umefika mwisho. Ametufunulia tabia Zake hasa katika wakati huu wa mwisho. Yeye ametupa mtazamo mmoja wa mwisho wa Uungu Wake mkuu wa neema. Wakati huu ni ufunuo wa jiwe la kifuniko wa nafsi Yake.

Mungu alikuja katika wakati huu wa Laodikia na kunena kupitia mwili wa mwanadamu. Sauti Yake imerekodiwa na kuhifadhiwa ili kumwongoza na kumkamilisha Bibi-arusi Neno Wake. Hakuna kabisa Sauti nyingine inayoweza kumkamilisha Bibi-arusi Wake ila Sauti Yake Mwenyewe.

Katika wakati huu wa mwisho, Sauti Yake iliyo kwenye kanda imewekwa kando; imetolewa nje ya makanisa. Hawataki tu kabisa kuzicheza kanda. Kwa hiyo Mungu anasema, “Mimi niko kinyume nanyi nyote. Nitawatapika mtoke katika kinywa Changu. Huu ni mwisho.”

“Kwa kuwa saba kati ya nyakati saba, sijaona kitu ila watu wakiliheshimu neno lao wenyewe kuliko Langu. Kwa hiyo mwishoni mwa wakati huu ninawatapika mtoke katika kinywa Changu. Yote yamekwisha. Nitazungumza basi. Naam, niko hapa katikati ya Kanisa. Amina wa Mungu, aliye mwaminifu na wa kweli atajifunua Mwenyewe na itakuwa KWA NJIA YA NABII WANGU.”

Kama ilivyokuwa hapo awali, wao wanafanya vile vile walivyofanya baba zao katika siku za Ahabu. Kulikuwa na jumla yao mia nne na wote walikubaliana; na wote wakisema jambo lile lile, waliwadanganya watu. Lakini nabii MMOJA, MMOJA TU, alikuwa sahihi na hao wengine wote walikuwa makosani kwa sababu Mungu alikuwa ametoa ufunuo kwa MMOJA TU.

Hii si kusema kwamba huduma zote ni za uongo na zinawadanganya watu. Wala Mimi sisemi mtu mwenye wito wa kuhudumu hawezi kuhubiri au kufundisha. Ninasema huduma tano ya KWELI itaweka KANDA, Sauti ya Mungu kwa Bibi-arusi, kuwa ndio Sauti iliyo muhimu sana UNAYOPASWA KUISIKIA. Sauti iliyo kwenye kanda ndio Sauti PEKEE ambayo imethibitishwa na Mungu Mwenyewe kuwa Bwana Asema Hivi.

Jihadharini na manabii wa uongo, kwa maana wao ni mbwa mwitu wakali.

Utajuaje kwa hakika njia sahihi kwa ajili ya siku hii? Kuna mgawanyiko jinsi hii miongoni mwa waaminio. Kundi moja la watu linasema huduma tano itamkamilisha Bibi-arusi, huku jingine linasema Bonyeza Play tu. Hatupaswi kugawanyika; tunapaswa kuungana kama BIBI-ARUSI MMOJA. Jibu sahihi ni lipi?

Hebu na tuifungue mioyo yetu pamoja na tusikie kile Mungu anachosema kwa Bibi-arusi kupitia nabii Wake. Kwa maana sote tunakubali, Ndugu Branham ndiye malaika-mjumbe Wake wa saba.

Juu ya msingi wa tabia za wanadamu peke yake, mtu ye yote anajua ya kwamba palipo na watu wengi kuna hata na maoni yasiyopatana juu ya mambo madogo-madogo ya fundisho muhimu ambalo wote wanashikilia pamoja. Ni nani basi atakayekuwa na mamlaka ya kutokosea ambayo itarudishwa katika wakati huu wa mwisho, kwa kuwa wakati huu wa mwisho utarudi kwenye kumdhihirisha Bibi-arusi wa Neno Halisi? Hiyo inamaanisha tutakuwa na Neno tena kama lilivyotolewa kikamilifu, na kueleweka kikamilifu katika siku za Paulo. Nitakwambia ni nani atakayekuwa nalo. Itakuwa ni nabii aliyethibitishwa kinaganaga, ama hata aliyethibitishwa kinaganaga zaidi kuliko nabii ye yote katika nyakati zote tangu Henoko hata siku hii, kwa sababu mtu huyu itambidi kuwa na huduma ya kinabii ya jiwe la kifuniko, na Mungu atamtambulisha. Haitambidi kujitetea, Mungu atamtetea kwa sauti ya ishara. Amina.

Hivyo, Ujumbe huu ulionenwa na mjumbe Wake ulitolewa kikamilifu, na unaeleweka kikamilifu.

Ni kitu gani kingine ambacho Mungu alichosema kumhusu malaika-mjumbe Wake wa saba na Ujumbe wake?

  • . Yeye atasikia tu kutoka kwa Mungu.
  • . Atakuwa na “Bwana asema hivi” na kunena kwa niaba ya Mungu.
  • . Yeye atakuwa kinywa cha Mungu.
  • . YEYE, KAMA INAVYOTANGAZWA KATIKA MALAKI 4:6, ATAIGEUZA MIOYO WA WATOTO IWAELEKEE BABA ZAO.
  • . Ata warudisha wateule wa siku za mwisho nao watamsikiliza nabii aliyethibitishwa akitoa kweli halisi kama vile ilivyokuwa kwa Paulo.
  • . Ata irudisha kweli kama walivyokuwa nayo.

Na kisha Yeye alisema nini kutuhusu sisi?

Na hao wateule walio pamoja naye katika siku hiyo watakuwa ndio wanaomdhihirisha Bwana kwa kweli na watakuwa ndio Mwili Wake na kuwa sauti Yake na kutenda kazi Zake. Haleluya! Unaliona hilo?

Kama ungali una mashaka yo yote juu ya jambo hili mwombe Mungu kwa Roho Wake akujaze na kukuongoza, kwa kuwa Neno linasema, “KWA MAANA WALIO WATEULE HAWAWEZI KUPUMBAZWA”. Hakuna mtu anayeweza kukupumbaza kama wewe ni Bibi-arusi.

Wakati Wamethodisti waliposhindwa, Mungu aliwainua wengine na kwa hiyo jambo hilo limeendelea kwa miaka mingi mpaka katika wakati huu wa mwisho kuna watu wengine nchini, ambao chini ya mjumbe wao watakuwa ndio sauti ya mwisho kwa wakati wa mwisho.

Naam bwana. Kanisa si “kinywa” cha Mungu tena. Ni kinywa chake lenyewe. Kwa hiyo Mungu analiacha. Ataliangamiza kupitia kwa nabii na bibi-arusi, kwa kuwa sauti ya Mungu itakuwa ndani ya bibi-arusi. Naam iko, kwa maana inasema katika sura ya mwisho ya Ufu. aya ya 17 “Roho na bibi-arusi wasema, njoo.” Mara nyingine tena ulimwengu utasikia moja kwa moja kutoka kwa Mungu kama ilivyokuwa wakati wa Pentekoste; lakini bila shaka huyo Bibi-arusi Neno atakataliwa kama ilivyokuwa katika wakati wa kwanza.

Bibi-arusi anayo sauti, bali itasema tu kile kilicho kwenye kanda. Kwa maana Sauti hiyo INATOKA MOJA KWA MOJA KWA MUNGU, hivyo haihitaji kufasiriwa kwa vile ilivyotolewa kikamilifu na inaeleweka kikamilifu.

Njoo uungane nasi Jumapili hii saa 06:00 SITA MCHANA, saa za Jeffersonville,(Ni Saa 2:00 MBILI USIKU ya Afrika Mashariki) tunapoisikia Sauti hiyo ikitufunulia: Wakati wa Kanisa la Laodikia 60-1211E.

Ndugu. Joseph Branham